Dodoma CC Mpira wa Mikono Wanaume yaichakaza Kwimba DC magoli 9–5 na kutinga Nusu Fainali SHIMISEMITA

Na. Mwandishi wetu, MBEYA

 

Timu ya Mpira wa Mikono ya Wanaume ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma imeonesha kiwango bora katika mashindano ya SHIMISEMITA yanayoendelea jijini Mbeya, baada ya kuibuka na ushindi wa magoli 9–5 dhidi ya Timu ya Halmashauri ya Wilaya ya Kwimba katika mchezo wa robo fainali.



Mchezo huo uliokuwa wa ushindani mkubwa na wenye mvuto mkubwa ulipigwa katika viwanja vya Shule ya Sekondari Samora, huku Timu ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma ikitawala mchezo na kutumia vema nafasi ilizopata hadi kufanikiwa kuondoka na ushindi huo muhimu.

 

Akizungumza mara baada ya kumalizika kwa mchezo huo, Kocha wa Timu ya Mpira wa Mikono ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Felician Rocky alisema kuwa ushindi huo ni matokeo ya maandalizi mazuri, nidhamu na juhudi kubwa zilizofanywa na wachezaji wake.

“Tumefanya vizuri katika mchezo huu. Wachezaji wameonesha moyo wa kupambana na kufuata maelekezo ya benchi la ufundi. Ushindi huu umetupa nguvu na kujiamini zaidi kuelekea mchezo wetu wa nusu fainali” alisema Rocky.

 


Kwa upande wake, mchezaji wa Timu ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Baraka Kasasi alisema kuwa  kufika hatua ya nusu fainali ni jambo kubwa kwa timu hiyo, lakini hawana mpango wa kuridhika na hatua hiyo.

“Tumefurahi sana kufika hatua hii, lakini bado safari yetu haijaisha. Tunakwenda kukutana na Timu ya Halmashauri ya Wilaya ya Chunya katika nusu fainali. Tumejipanga vizuri na tunaamini tutaivuka hatua hiyo na kuelekea katika hatua inayofuata ambayo ni fainali na tunaendelea kupambana hadi tufikie malengo yetu ya kuwania ubingwa” alisema Kasasi.

 


Ushindi wa magoli 9–5 dhidi ya Timu ya Halmashauri ya Wilaya ya Kwimba umeongeza matumaini kwa Timu ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma, huku macho ya mashabiki sasa yakielekezwa katika mchezo wa nusu fainali dhidi ya Timu ya Halmashauri ya Wilaya ya Chunya

Comments

Popular Posts

Vijana watakiwa kujiendeleza nje ya mfumo rasmi

NGOs zatakiwa kuzingatia uwazi na uwajibikaji Dodoma