Timu ya Watumishi Jiji la Dodoma inayoshiriki SHIMISEMITA yatakiwa kurejea na ushindi
Na. Lulu Luvanda, DODOMA
Timu ya watumishi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma
itakayoshiriki Mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Serikali za Mitaa
Tanzania (SHIMISEMITA) wametakiwa kulitangaza vema jiji hilo katika michezo kwa
kuzingatia nidhamu na misingi ya utumishi wa umma na kurejea na ushindi.
Kauli hiyo ilitolewa na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Dkt. Frederick Sagamiko wakati wa tukio la kuwaaga wanamichezo hao watakaoshiriki michezo ya SHIMISEMITA jijini Mbeya.
Akizungumza katika hafla ya kuwaaga wachezaji hao iliyofanyika
katika ukumbi wa halmashauri jijini Dodoma, alisema kuwa mashindano hayo ni
fursa ya kulitangaza Jiji la Dodoma kupitia michezo, huku akiwataka wachezaji
kuzingatia nidhamu, maadili na misingi ya utumishi wa umma.
Alitumia hafla hiyo kumpongeza Kaimu Mkuu wa Kitengo
cha Michezo, Utamaduni na Sanaa, Neema Kilongola kwa mchango wake katika
kuimarisha michezo ndani ya halmashauri hiyo, akisisitiza kuwa mafanikio ya
timu yanaongeza utambulisho wa Dodoma kitaifa.
Kwa upande wake Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Michezo,
Utamaduni na Sanaa alisema kuwa timu hiyo imejiandaa vizuri na kwamba lengo lao
si kushiriki pekee, bali kupigania ushindi. Alisema kuwa maandalizi yamejikita
katika kuimarisha maeneo yaliyokuwa na changamoto pamoja na kuongeza uwezo na
ushirikiano wa wachezaji.
Akizungumza kwa niaba ya wachezaji, mchezaji
mwandamizi, Leonard Mkinga alisema kuwa timu imejiandaa vizuri na ina dhamira
ya kurejea Dodoma na matokeo mazuri, akitaja nia, maandalizi na nidhamu kuwa
nguzo muhimu ya mafanikio.
Timu hiyo ina wachezaji 60 inatarajiwa kushiriki
mashindano hayo kwa siku 15, ikikabiliana na timu kutoka halmashauri mbalimbali
nchini.
Comments
Post a Comment