Dodoma CC yaangukia msindi wa pili Mpira wa Wavu Wanaume SHIMISEMITA

Na. Leah Mabalwe, MBEYA

 

TIMU ya Mpira wa Wavu ya Wanaume kutoka Halmashauri ya Jiji la Dodoma imeibuka mshindi wa pili katika mashindano ya Fainali za SHIMISEMITA, baada ya kukubali kichapo cha Seti 3-0 kutoka kwa Manispaa ya Iringa katika mchezo wa fainali uliochezwa kwenye Uwanja wa Shule ya Sekondari Samora.

 


Mchezo huo wa fainali ulikuwa wa ushindani mkubwa, huku timu zote zikionesha kiwango kizuri cha mchezo na kupambana kutwaa ubingwa wa mashindano hayo.

Kocha wa Timu ya Mpira wa Wavu ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Wanjala Matinya alisema kuwa timu yake ilijiandaa vizuri hadi kufikia hatua ya fainali, lakini pia wapinzani wao walikuwa wamejiandaa ipasavyo na kuweza kupata ushindi.

 “Tumejiandaa vizuri hadi kufikia hatua ya fainali. Lakini wapinzani wetu nao walikuwa wamejiandaa vizuri, ndiyo maana wameweza kupata ushindi” alisema Matinya.

Kwa upande wake, mchezaji wa Timu ya Mpira wa Wavu, Galucy Kyando alisema kuwa mchezo huo ulikuwa wa ushindani wa hali ya juu kwa sababu kila timu ilihitaji kuondoka na ushindi.

Kyando alisema kuwa licha ya kutwaa nafasi ya pili, matokeo hayo si mabaya kwa timu yao, kwasababu kufika fainali ni ishara kwamba timu imeonesha uwezo na ushindani katika mashindano hayo.

“Mpira ulikuwa wa ushindani wa hali ya juu kwa sababu kila timu ilitaka kuwa ya kwanza. Sisi tumeibuka washindi wa pili, na nafasi hii si mbaya” alisema Kyando.

 

Kwa matokeo hayo, Manispaa ya Iringa imeandika historia ya kutwaa ubingwa wa Mpira wa Wavu wa Wanaume katika Fainali za SHIMISEMITA, huku Halmashauri ya Jiji la Dodoma ikijihakikishia nafasi ya pili baada ya safari nzuri iliyowafikisha katika mchezo wa mwisho wa mashindano.

Comments

Popular Posts

Vijana watakiwa kujiendeleza nje ya mfumo rasmi

NGOs zatakiwa kuzingatia uwazi na uwajibikaji Dodoma

Uendelevu wa NGOs wapatiwa msukumo wilayani Dodoma