Bonanza la Michezo lahamasisha Wananchi kuboresha taarifa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura Jiji la Dodoma
Na. Nancy Kivuyo, UHURU
Halmashauri
ya Jiji la Dodoma yafanya bonanza la michezo la hamasa kuelekea Uboreshaji wa Daftari
la Kudumu la Mpiga Kura awamu ya pili kwa lengo la kuhamasisha wananchi
kujitokeza kujiandikisha ili wapate haki ya kupiga kura ifikapo mwezi Oktoba,
2025.
Hayo yalisemwa na Afisa Mwandikishaji Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Dickson Kimaro kabla ya ufunguzi wa bonanza la hamasa kuelekea Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura katika uwanja wa michezo wa Mtekelezo katika Kata ya Uhuru, jijini Dodoma.
Alisema
kuwa lengo la bonanza hilo ni kuwahamasisha wananchi kujitokeza kwenda
kujiandikisha ili wapate fursa ya kupiga kura. “Tunategemea kufanya maboresho
ya uandikishaji katika Daftari la Kudumu la Mpiga Kura ili watu wapate sifa ya
kupiga kura hapo mwezi Oktoba, 2025. Halmashauri ya Jiji la Dodoma ina vituo
105 na uandikishaji unategemewa kuanza mnamo tarehe 16 – 22 Mei, 2025” alisema
Kimaro.
Aliongeza
kuwa vituo vitakuwa wazi kuanzia saa mbili asubuhi na kufungwa saa kumi na
mbili jioni na wanatilia mkazo hamasa kuwa wananchi wenye sifa wajitokeze.
“Wapiga kura wapya ambao wametimiza miaka 18 na wale ambao hadi mwezi Oktoba,
2025 watakuwa wamefikisha miaka 18 wanaruhusiwa kujiandikisha. Hata wale ambao
hawakuwahi kujiandikisha nao wanapaswa kujiandikisha na wale wanaohuisha
taarifa zao za makazi kutoka eneo moja na wamehamia eneo jingine wanapaswa
kwenda kubadili taarifa zao ili wapate haki yao ya msingi ya kupiga kura”
aliongeza Kimaro.
Katika
hatua nyingine alihimiza vijana wenye sifa kujitokeza ili wapate haki yao ya
msingi ya kupiga kura ili kuchagua viongozi bora. “Katika bonanza hili
mnajionea wenyewe kundi kubwa lililopo hapa ni vijana, wameonesha mwitikio
mkubwa na hawa tunatamani sana wapate hamasa hii ili wakajiandikishe na
hatimaye waweze kushiriki katika upigaji kura” alihimiza Kimaro.
Naye
mwananchi wa mtaa wa kati, Kata ya Uhuru, Hamida Kapela alisema kuwa
amejiandikisha katika awamu ya kwanza kwasababu anatambua umuhimu wa kupiga
kura. “Mimi nimejiandikisha tangu mwanzo wa zoezi, nimekitunza kitambulisho
changu na nimatumaini mwezi Oktoba, 2025 nitapiga kura kumchagua kiongozi bora
atakeendeleza mazuri ambayo serikali inatufanyia” alisema Kapela.
Alihimiza
wananchi wa Kata ya Uhuru na Jiji zima la Dodoma hasa wale ambao
hawakujishughulisha na zoezi la uandikishaji kujitokeza kujiandikisha ili
wapate nafasi ya kupiga kura muda utakapofika. “Nawasisitiza wananchi wenzangu,
akina mama, vijana na wale wote wenye vigezo vya kupata kadi ya mpiga kura
nendeni mkajiandikishe ili mpate haki yenu ya kikatiba ya kupiga kura na
kumchagua kiongozi bora unayemtaka” alihimiza Kapela.
Kwa
upande wake Afisa Mwandikishaji Msaidizi ngazi Kata, Kata ya Uhuru, Fatuma Amri
alieleza kuwa zoezi la uhamasishaji awamu ya pili linafanyika ili kuwasaidia
wale ambao hawakujiandikisha wajitokeze wakajiandikishe. “Katika kata yangu,
wananchi wengi ni wafanyabiashara na muda mwingi wanakosa muda wa kutoka lakini
nawahimiza kuwa waende wakajiandikishe ili baadaye waweze kupiga kura na
kuchagua viongozi wao. Nawahimiza pia vijana wa bodaboda nao wasibaki nyuma
mkajiandikishe ili mwezi Oktoba mpige kura ili mpate viongozi watakaoleta
maendeleo” alieleza Amri.
Zoezi
la Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Mpiga Kura linatarajiwa kufunguliwa
kuanzia tarehe 16-22 Mei, 2025 katika Halmashauri ya Jiji Dodoma na
linatarajiwa kuwa na vituo 105 vitakavyofunguliwa kuanzia saa mbili asubuhi na
kufungwa saa kumi na mbili jioni.
MWISHO
Comments
Post a Comment