Utunzaji Mazingira Kata ya Kilimani kielelezo bora cha kuigwa

Na. Nancy Kivuyo, KILIMANI

Kata ya Kilimani yaendelea kuhimiza kwa vitendo utunzaji wa mazingira kwa kupanda miti mbalimbali ikiwemo ya kivuli pamoja na matunda ili kuweka mazingira safi na ya kuvutia jambo linalowafanya wananchi wake kufurahia mandhari na kuwa na lishe bora.




Akizungumza na waandishi wa habari waliotembelea kata hiyo kujionea utunzaji wa mazingira unavyofanyika Diwani wa Kata ya Kilimani, Neema Mwaluko alisema kuwa wanajitahidi kupanda miti ili kuweka mazingira katika hali nzuri inayovutia. “Sisi hapa Kilimani tuna program za kupanda miti kila mwaka. Ofisi ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma kila mwaka inatupatia miche ya miti kwaajili ya kupanda katika kata yetu” alisema Diwani Mwaluko.

Aliongeza kuwa wanatoa elimu ya utunzaji mazingira kwa wananchi wa kata hiyo ili kuhakikisha wanakuwa vinara na mfano wa kuigwa katika Jiji la Dodoma. “Kwa ujumla kata yetu inafanya vema katika utunzaji wa mazingira. Kama mnavyojionea sehemu kubwa ni kijani, kila kaya unayoona ina miti na mazingira yanavutia. Tutaendelea kuwaelimisha wananchi kutunza mazingira ili yatufae sote na vizazi vijavyo” aliongeza Diwani Mwaluko.

Naye mwananchi wa Kata ya Kilimani, Jonasi Masanika alisema kuwa wamenufaika na uongozi uliopo kwasababu unawahamasisha kutunza mazingira. “Kipekee niwashukuru viongozi wa kata, wanatuelimisha na kutuhamasisha kupanda miti na kutunza mazingira. Vijana tunahusika sana katika kupokea elimu hiyo na tunaishukuru sana serikali kwa kutubeba hata katika masuala kama haya” alishukuru Masanika.

Kata ya Kilimani ni miongoni mwa kata 41 zilizopo katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma. Kata hiyo ina jumla ya wakazi 9,562 ambapo wanaume ni 4,609 na wanawake ni 4953. Shughuli zinazofanyika ni kilimo na ufugaji na shughuli za kiuchumi ni biashara za jumla na rejareja na ujasiriamali.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Jiji la Dodoma lapewa angalizo lishe bora kwa wananchi

RC Dodoma apongeza wafugaji kwa ushiriki wa Paredi ya Mifugo

Rais Samia: Tumieni kikamilifu Miundombinu, Teknolojia na mitaji iliyowekezwa katika Kilimo, Uvuvi na Mifugo