Shule mpya ya Msingi Chinyoyo ya kwanza kujengwa Kata ya Kilimani

Na. Emmanuel Charles, KILIMANI

Mradi wa ujenzi wa shule mpya ya Chinyoyo, Kata ya Kilimani unaogharimu shilingi 147,000,000 ni shule ya kwanza kujengwa katani hapo na itaondoa adha ya wanafunzi ya kutembea umbali mrefu kufuata masomo.




Haya yalisemwa na Diwani wa Kata ya Kilimani, Neema Mwaluko wakati akizungumza na waandishi wa habari waliofanya ‘Media Tour’ kukagua miradi ya maendeleo iliyotekelezwa na serikali kuanzia 2021-2025 katika kata hiyo.

Alisema kuwa kwasababu kata yake ipo mjini, miundombinu ikiwemo ya elimu ilichelewa kufika na sasa serikali ya awamu ya sita inajenga shule ya msingi ili kuwakwamua watoto wanaotembea umbali mrefu. “Kwa miaka yote ya nyuma, kata hii haikuwahi kuwa na shule yeyote na wanafunzi wanalazimika kutembea umbali mrefu kufuata masomo katika kata za jirani. Tunaishukuru serikali ya awamu ya sita kwa kutuona na kuamua kutenga eneo la kujenga Shule ya Msingi Chinyoyo kwa gharama ya shilingi 147,000,000 ambapo ujenzi wa madarasa manne na ofisi mbili umegharimu shilingi 110,000,000, matundu 10 ya vyoo shilingi 17,000,000 na uchimbaji wa kisima shilingi 20,000,000. Shule hii itakapokamilika tunaamini itakuwa mkombozi kwa wanafunzi wa kata hii hasa wale wadogo hawatatembea tena kwenda mbali” alisema Diwani Mwaluko.

Aliongeza kuwa ujenzi wa mradi huo utapunguza adha nyingi zilizokuwa zinawakabili watoto na kuwapa nafasi ya kufurahia upatikanaji wa elimu bora katika shule hiyo. “Watoto wa kata hii walikua wanakumbwa na adha nyingi sana ikiwemo utoro na kutokuwepo usalama wa watoto wanapokuwa wanatembea wenyewe. Niwahakikishie wananchi kuwa uwepo wa shule hii utawasaidia watoto kusoma vizuri na hizo changamoto zilizokuwepo mwanzoni zitapungua na hatimaye kuisha kabisa. Tunamshukuru Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma kwa upendeleo huu na kiwanja cha eneo hili la shule kimeshapimwa. Hivyo, tutasimamia mradi huu ukamilike kwa wakati ili watoto waanze masomo mara moja” aliongeza Diwani Mwaluko.




Kwa upande mwingine Diwani Mwaluko alisema kuwa katika eneo hilo yapo maeneo yameshapimwa kwaajili ya ujenzi wa shule ya sekondari, kituo cha polisi na kituo cha afya ambapo miundombinu hiyo itasaidia kwa uteshelevu mahitaji ya wakazi wa Kilimani.

Naye Afisa Mtendaji wa Mtaa Chinyoyo, Happyness Japhet alieleza kuwa serikali ya awamu ya sita imefanya vizuri sana kujenga shule hiyo kwasababu itawasaidia wanafunzi kusoma karibu na kupata elimu bora. “Serikali yetu ni sikivu imeweza kusikiliza kilio cha wananchi na kujenga shule hii. Watoto wadogo wa shule ya awali walikua wanataseka kuamka alfajiri na kutembea umbali mrefu kufuata shule. Shule hii ni mkombozi wa wananchi wa Chinyoyo na changamoto zote zitabaki historia. Hongera nyingi kwa serikali yetu sikivu” alieleza Japhet.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Jiji la Dodoma lapewa angalizo lishe bora kwa wananchi

RC Dodoma apongeza wafugaji kwa ushiriki wa Paredi ya Mifugo

Rais Samia: Tumieni kikamilifu Miundombinu, Teknolojia na mitaji iliyowekezwa katika Kilimo, Uvuvi na Mifugo