WAKAZI WA NALA WAADHIMISHA MIAKA 62 YA MUUNGANO KWA KUSHIRIKI USAFI WA MAZINGIRA

Na. Mwandishi Wetu, NALA - DODOMA

WAKAZI wa Mtaa wa Barazani, Kata ya Nala wamejitokeza kwa wingi katika zoezi la usafi wa mazingira linalofanyika kila Jumamosi ya mwisho wa mwezi kwa lengo la kuendelea kuhakikisha mji unakuwa safi na kujenga mazoea ya kupenda kufanya usafi.



Zoezi hilo la usafi limekuwa la kipekee kwasababu limefanyika sambamba na kuadhimisha Miaka 62 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, ambapo wananchi walionekana wenye hamasa kubwa katika kuboresha muonekano wa mtaa wao.

Akizungumza na wakazi ho mara baada ya zoezi la usafi kukamilika, Afisa Mazingira kutoka Kanda Namba Tatu, Neema Komba aliwapongeza wananchi kwa kujitokeza kwa wingi na kuonesha uthamani wa kuishi katika mazingira safi. “Leo tumefanya jambo jema sana kujitokeza kufanya usafi, kwanza tumetimiza ule wajibu wetu wa kufanya usafi kila jumamosi ya mwisho wa mwezi lakini pia tupo hapa kuadhimisha kwa umoja wetu miaka 62 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar. Muungano huo unaendelea kutukumbusha kushirikiana na kusaidiana ili nchi yetu iendelee kuwa na amani. Ushiriki huu ni ishara ya ukomavu wa kijamii na uwajibikaji katika kutunza afya za wakazi wa Nala” alisema Komba.

Aidha, Aliwahimiza wananchi kuendeleza utamaduni wa kufanya usafi kila wakati ili kuepuka magonjwa ya mlipuko yanayotokana na uchafu. Alisisitiza kuwa mazingira bora ni msingi wa afya imara na kila mwananchi anapaswa kuwa mlinzi wa mwenzake kwa kuhakikisha maeneo yanayowazunguka yanabaki kuwa salama na safi.

Nae, Afisa Mtendaji wa Mtaa wa Nala, Alinikisia Humbo alisema kuwa usafi wa mazingira unapaswa kufanyika bila shuruti ili kuepuka taka zinazozagaa hovyo katika mitaa ambazo ni hatari kwa afya za wakazi. “Naomba kuwakumbusha kuwa usafi wa mazingira ni suala muhimu sana. Mmejionea taka zilizokuwa zimezagaa hapa, tusaidiane katika kukemea wale wanaotupa taka bila utaratibu ili tuwadhibiti kwasababu ndio wanafanya taswira ya jiji letu kuonekana chafu. Ifike mahala tuone aibu kutupa taka hovyo, tuyatunze mazingira ili nayo yatutunze na vizazi vijavyo” alisema Humbo.

Zoezi hilo la usafi wa mazingira lilikuwa mahsusi kwa ajili ya kuuenzi Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ambao unatarajiwa kuadhimishwa tarehe 26 Aprili, 2026 ukiwa na kaulimbiu isemayo “Miaka 62 ya Muungano: Amani, Umoja na Mshikamano ni Msingi wa Maendeleo Endelevu.












MWISHO

 

Comments

Popular Posts

Juhudi na nidhamu yatakiwa kwa washiriki wa mafunzo ya Jeshi la Akiba Dodoma

Wanafunzi Dodoma watakiwa kutoa taarifa za ukatili wa kijinsia