KANDA NAMBA MBILI YAADHIMISHA MIAKA 62 YA MUUNGANO WA TANGANYIKA NA ZANZIBAR KWA KUFANYA USAFI WA JUMAMAMOSI YA MWISHO WA MWEZI

Na. Tutindaga Nkwindi, DODOMA

KANDA Namba Mbili imeadhimisha miaka 62 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar kwa kufanya zoezi la usafi katika Kata ya Nzuguni, Mtaa wa Nzuguni A pamoja na Kituo Kikuu cha Mabasi Dodoma ikiwa ni sehemu ya kuenzi umoja na mshikamano wa watanzania.




Zoezi hilo liliongozwa na Meneja wa Kanda Namba Mbili, Hussen Nyenye aliyeshirikiana na watumishi wa kanda hiyo pamoja na wananchi kusafisha mazingira katika maeneo hayo muhimu ya jiji.

Akizungumza wakati wa zoezi hilo aliwashukuru Kikundi cha Wanawake wa Stendi maarufu kama Malkia wa Nguvu kwa kujitokeza kwa wingi kushiriki usafi huo. “Nawapongeza sana Malkia wa Nguvu kwa kuungana nasi kusafisha eneo hili muhimu ikiwa ni moja ya njia za kuadhimisha muungano wetu huku tukizingatia kaulimbiu ya mwaka huu isemayo ‘Miaka 62 ya Muungano: Amani, Umoja na Mshikamano ni Msingi wa Maendeleo Endelevu'. Pia tukumbuke kuwa mazingira safi ndiyo msingi wa kila kitu katika maendeleo ya jamii” alisema Nyenye.

Kwa upande wake, mwanachama wa Kikundi cha Malkia wa nguvu Subira Mtandi alisema kuwa wanawake wanaofanya kazi katika Kituo Kikuu cha Mabasi Dodoma wameona umuhimu wa kuuenzi muungano kwa vitendo. “Sisi wanawake tunaofanya kazi hapa stendi, tumeamua kuuenzi muungano wetu kwa kufanya usafi katika eneo letu la kazi ili kudumisha mazingira bora” alisema Mtandi.

Nae, Afisa Mazingira wa Kanda Namba Mbili, Neema Mbawala aliwashukuru wakazi wa Mtaa wa Nzuguni A kwa kujitokeza kushiriki zoezi la usafi, akieleza kuwa usafi ni njia mojawapo ya kuimarisha mshikamano na kuadhimisha muungano kwa vitendo.

Maadhimisho hayo yameonesha umuhimu wa ushirikiano kati ya viongozi na wananchi katika kulinda mazingira, huku yakisisitiza kuwa amani, umoja na mshikamano vinabaki kuwa nguzo kuu ya maendeleo endelevu ya taifa.







MWISHO 

 

 

Comments

Popular Posts

Juhudi na nidhamu yatakiwa kwa washiriki wa mafunzo ya Jeshi la Akiba Dodoma

Wanafunzi Dodoma watakiwa kutoa taarifa za ukatili wa kijinsia