KAMATI YA KUDHIBITI UKIMWI KUTOA ELIMU YA KINGA KWA VIJANA DODOMA
Na. Mwandishi Wetu, DODOMA
Kamati
ya Kuzuia na Kudhibiti UKIMWI ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwa kushirikiana
na Taasisi ya DOYODO imeendelea kutoa elimu na mafunzo kwa jamii, hususan kwa
vijana, ili kuhakikisha wanapata uelewa sahihi wa namna ya kujikinga na ugonjwa
huo.
Hayo aliyasema Mwenyekiti wa ALAT Mkoa wa Dodoma (WASEMI), Leticia Sanga tarehe 29 Aprili, 2026 wakati alipokuwa akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa shughuli za kudhibiti UKIMWI kwa kipindi cha robo ya tatu kuanzia Januari hadi Machi, 2026 katika Mkutano wa Baraza la Madiwani uliofanyika katika ukumbi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma.
Alisema
kuwa juhudi hizo zimeanza kuzaa matunda, lakini bado kuna haja ya kupanua wigo
wa elimu hiyo. “Tumekuwa tukiwalenga zaidi vijana, lakini sasa tumeona umuhimu
wa kuwafikia pia wazee. Wazee wengi wamekuwa waathirika wakubwa wa janga hili
kwa sababu wanabeba jukumu la kuwahudumia watoto wao wanaoishi na virusi vya
UKIMWI. Hivyo, nao wanahitaji elimu hii kwa kina zaidi” alisema Sanga.
Kwa
upande wake, Diwani wa Kata ya Chahwa, Jorome Petro alisisitiza umuhimu wa
kupeleka elimu hiyo katika maeneo ya pembezoni mwa Halmashauri ya Jiji la
Dodoma, akieleza kuwa bado kuna upungufu mkubwa wa uelewa katika maeneo hayo.
“Elimu
hii isiishie katikati ya jiji pekee. Tuendelee kuwafikia wananchi wa kata za
pembezoni ambao mara nyingi hukosa taarifa sahihi na hivyo kubaki nyuma katika
mapambano haya. Hivyo, naomba elimu hii iwafikie na waliopo pembezoni mwa mji”
alisema Petro.
Naye
Mstahiki Meya wa Jiji la Dodoma, Alimwoni Chaula, alitoa wito kwa wadau wote
kutumia vema fursa ya Mbio za Mwenge wa Uhuru kueneza elimu dhidi ya mapambano
ya UKIMWI kwa jamii kupitia vyombo vya habari.
“Tunapoelekea
kwenye Mbio za Mwenge wa Uhuru tutumie nafasi hii katika kutoa elimu kwa dhamira
ya kutumia kila jukwaa, hususan vyombo vya habari, kuelimisha jamii kuhusu
namna ya kujikinga na UKIMWI. Elimu ndiyo silaha kuu ya kumaliza janga hili”
alisema Chaula.
Baraza
la Madiwani la Halmashauri ya Jiji la Dodoma lilisisitiza ushirikiano wa wadau
mbalimbali na utoaji endelevu wa elimu kwa makundi yote ya jamii ni msingi
muhimu katika kufikia lengo la kutokomeza UKIMWI nchini.
MWISHO
Comments
Post a Comment