Kata ya Mnadani yahimizwa kuzingatia usafi wa Mazingira

 Na. Mwandihsi wetu, MNADANI

Diwani wa Kata ya Mnadani, Mugendi Kerenge amewakumbusha wananchi wa Mtaa wa Mnadani kuzingatia usafi wa mazingira ikiwemo utoaji wa taka mapema na pia ulipaji wa ada ya taka ambayo ni mapato ya halmashauri.





Aliyazungumza hayo katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika Mtaa wa Mnadani jijini Dodoma.

Alisema kuwa usafi wa mazingira unafanywa ili kujikinga na magonjwa pamoja na kuboresha mandhari ya eneo husika. Pia alisisitiza kuwa usafi wa mazingira ni jukumu la kila mwananchi na si la serikali pekee. "Ni wajibu wetu sote kuhakikisha mazingira yanakuwa safi wakati wote. Tukifanya hivyo, tutajikinga na magonjwa ya mlipuko na kuongeza hadhi ya mtaa wetu, niwatake vikundi vinavyohusika katika uondoshaji wa taka kwenye kata hii muwe na ratiba ambayo itamjulisha mwanchi ni siku gani mtapita katika mtaa anaoishi" alisema Kerenge.

Aidha, aliwataka wananchi kuacha tabia ya kutupa taka hovyo na badala yake kutumia maeneo maalum yaliyotengwa kwa ajili ya ukusanyaji wa taka, huku akisisitiza umuhimu wa kushiriki katika shughuli za usafi wa pamoja. “Nitoe rai kwa wananchi kuwa ada ya taka ni lazima kwahiyo kwa yeyote asiyetoa atalipishwa faini kulingana na sheria ndogo za mazingira maana baadhi ya wananchi wamekuwa wakikiuka sheria hizi” alisema Kerenge.





Kwa upande wake Mwananchi wa Mtaa wa Mnadani, Mwadawa Omari alisema kuwa changamoto ya ukusanyaji wa taka bado ipo katika maeneo yao, wakiiomba serikali ya mtaa kuboresha huduma hiyo ili kuwezesha mazingira kuwa safi zaidi.

Alishauri kuwa, wahusika wanaoondosha taka kwenye mitaa wazingatie ratiba kwasababu taka zikikaa muda mrefu husababisha harufu ambayo inaleta kero kwa wananchi na wapita njia.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Gari la Darasa Tembezi latoa elimu Mitaa ya Jiji la Dodoma

Dodoma Jiji FC yatangaza benchi la ufundi msimu wa 2025/2026

Kata ya Chamwino kipaumbele Lishe shuleni