Wamiliki wa Viwanja watakiwa kuvisafisha na kuviendeleza Dodoma

 

Na. Mwandishi Wetu, DODOMA

HALMASHAURI ya Jiji la Dodoma imewataka wananchi na taasisi kusafisha, kuendeleza na kulinda mipaka ya viwanja vyao na kueleza kuwa kushindwa kufanya hivyo, vitatolewa kwa watu wengine wenye uhitaji wa viwanja kwa mujibu wa sheria.




Akizungumza na waandishi wa habari, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Dennis Gondwe alisema kuwa wananchi na wamiliki wote wa viwanja wana wajibu wa kusafisha viwanja vyao. “Ndugu waandishi wa habari, Halmashauri ya Jiji la Dodoma inapenda kuwataarifu wananchi wote pamoja na taasisi ambazo zinamiliki viwanja ndani ya Jiji la Dodoma kuendeleza viwanja hivyo kwa mujibu wa Sheria ya Ardhi Namba 4 ya Mwaka 1999 (Sura ya 113). Sheria hiyo, inawataka wananchi wote pamoja na taasisi zinazomiliki viwanja kuviendeleza viwanja hivyo ndani ya muda usiozidi miezi 36 tangu walipokabidhiwa au kumilikishwa” alisema Gondwe. 

Alisema kuwa limeibuka wimbi la watu wasio na nia njema wanaovamia viwanja ambavyo havijasafishwa, kuendelezwa na kujimilikisha viwanja hivyo. “Aidha, wananchi wengine wamefikia hatua ya kung’oa ‘beacons’ na kusababisha usumbufu mkubwa kwa wamiliki wa viwanja hivyo kwa mujibu wa sheria kwa upande mmoja, na kwa upande mwingine usumbufu kwa halmashauri ambayo ndiyo mamlaka ya upangaji, upimaji na umilikishaji. Vilevile, kumekuwa na wimbi la kuvamia mipaka ya viwanja katika baadhi ya maeneo. Nitumie hadhira hii kuwataarifu kuwa haya ni makosa kama yalivyo makosa mengine” alisema.

 


Akitoa kauli rasmi ya halmashauri alisema kuwa kila mmiliki wa kiwanja anapaswa kutimiza wajibu wake kwa mujibu wa sheria. “Kwa Ilani hii, Halmashauri ya Jiji la Dodoma inawataka wananchi wote na taasisi zote kulinda mipaka ya viwanja vyao, kuendeleza viwanja au maeneo yao kwa mujibu wa sheria. Kutofanya hivyo, halmashauri itaendelea na taratibu za kufuta miliki hizo kwa mujibu wa sheria” alisema Gondwe.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Gari la Darasa Tembezi latoa elimu Mitaa ya Jiji la Dodoma

Dodoma Jiji FC yatangaza benchi la ufundi msimu wa 2025/2026

Kata ya Chamwino kipaumbele Lishe shuleni