Jiji la Dodoma lashauriwa kulinda hadhi ya Makao Makuu ya Nchi
Na. Mwandishi wetu, DAR ES SALAAM
HALMASHAURI
ya Jiji la Dodoma imeshauriwa kuendelea kusimamia Mpango Kabambe wake ili
kuhakikisha jiji linakuwa na mpangilio wa kisasa na kulinda hadhi ya makao
makuu ya nchi.
Katibu Mkuu Ofisi ya Rais, Maendeleo ya Vijana, Jenifa Omolo (kushoto) akiongea na wataalam wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma
Kauli
hiyo ilitolewa na Katibu Mkuu Ofisi ya Rais, Maendeleo ya Vijana, Jenifa Omolo
alipotembelea banda la Halmashauri ya Jiji la Dodoma katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa
ya Biashara Sabasaba yanayoendelea katika viwanja vya Mwl. Julius Nyerere
jijini hapa.
Alisema
kuwa ukuaji wa Jiji la Dodoma unapaswa kwenda sambamba na upangaji bora wa
maeneo, miundombinu na mazingira ya mji ili kuongeza mvuto zaidi kwa wakazi,
wawekezaji na wageni wanaofika kwa shughuli mbalimbali za kiserikali na
kiuchumi.
Alisisitiza
kuwa taswira ya mji ambao ni makao makuu ya nchi inapaswa kuonekana wazi
kupitia mpangilio wa kisasa, unaozingatia uzuri wa mji, matumizi sahihi ya
ardhi na maendeleo yanayopangika na yanapaswa kuendana na kutenga maeneo ya
shughuli za kiuchumi za vijana ambao ndio taifa la kesho.
Hivyo,
utekelezaji wa Mpango Kabambe wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma ni jambo muhimu
sana kwa mustakabali wa sasa na wa kesho.
Kwa
upande wake, mwananchi aliyetembelea banda la Halmashauri ya Jiji la Dodoma
katika Maonesho ya Sabasaba, Omary Nyange alisema kuwa amefurahia kupata majibu
ya maswali yake kuhusiana na fursa za viwanja katika jiji hilo. Aidha, aliipongeza
Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwa kushiriki katika maonesho hayo.
Halmashauri ya Jiji la Dodoma
inashiriki katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa (Sabasaba)
yanayofanyika katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, jijini Dar es Salaam,
kuanzia tarehe 28 Juni hadi 13 Julai 2026 chini ya kaulimbiu isemayo “Maonesho
ya Biashara ya Kimataifa Sabasaba ni Fahari ya Tanzania”.
Comments
Post a Comment