Timu ya Watumishi Jiji la Dodoma yadaiwa ushindi mashindano ya SHIMISEMITA
Na. Lulu Luvanda, DODOMA
Halmashauri ya Jiji la Dodoma imeiaga timu ya
watumishi itakayoliwakilisha jiji hilo katika Mashindano ya Shirikisho la
Michezo ya Serikali za Mitaa (SHIMISEMITA) 2026 yatakayofanyika jijini Mbeya na
kutakiwa kurejea na ushindi.
Kauli hiyo ilitolewa na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Dkt. Frederick Sagamiko alipokuwa akiiaga timu hiyo katika ukumbi wa mikutano wa halmashauri.
Akizungumza katika hafla ya kuwaaga wachezaji hao
jijini Dodoma, alisema kuwa mashindano hayo ni fursa ya kulitangaza Jiji la
Dodoma kupitia michezo, huku akiwataka wachezaji hao kuzingatia nidhamu,
maadili na misingi ya utumishi wa umma.
Aliwakumbusha umuhimu wa michezo katika kuimarisha
afya, mshikamano na uhusiano miongoni mwa watumishi, huku akiwataka kulitangaza
vizuri Jiji la Dodoma kwa kuonesha uwezo, nidhamu na ushindani wa hali ya juu.
Kwa upande wake Meneja wa Timu ya watumishi wa Jiji la Dodoma, Dkt. Sebastian Pima alisema kuwa wamefurahia kumuona Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma akikutana na timu nzima na kuwapa maneno ya hamasa kabla ya kuelekea kwenye mashindano ya SHIMISEMITA. Aliishukuru ofisi ya mkurugenzi kwa uungaji mkono unaotolewa kwa timu hiyo, hatua inayochochea maandalizi na hamasa kubwa ya kushiriki kwa lengo la kupata ushindi.
Alisema kuwa wanatambua Dodoma ni Fahari ya
Watanzania, hivyo timu pamoja na safu ya uongozi ipo tayari kuhakikisha
inaiwakilisha na kuifaharisha Dodoma katika mashindano hayo. Alisisitiza kuwa
umoja, maandalizi na dhamira ya ushindi ni muhimu katika kufanikisha lengo
hilo.
Akizungumza kwa niaba ya wachezaji wenzake, mchezaji
mwandamizi Leonard Mkinga alisema kuwa timu imejiandaa vizuri ikiwa na dhamira
ya kurejea Dodoma na matokeo mazuri. Alisema kuwa nia, maandalizi na nidhamu
kuwa nguzo muhimu za mafanikio.
Timu hiyo yenye jumla ya wachezaji 60 inatarajiwa
kushiriki mashindano hayo kwa siku 15, kuanzia tarehe 16 Agosti, hadi tarehe 28
Agosti, 2026.
Comments
Post a Comment