ILEMELA MANISPAA YAVUTIWA UWEKEZAJI MIRADI YA KIMKAKATI DODOMA
Na. Tutindaga Nkwindi, DODOMA
MADIWANI wa Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela wamevutiwa na
uwekezaji na utekelezaji wa miradi ya kimkakati inayotekelezwa na Halmashauri
ya Jiji la Dodoma na kulitaja kuwa ni jiji darasa.
Kauli hiyo ilitolewa na Naibu Meya wa Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela, Kuruthum Abdallah baada ya kutembelea miradi ya kimkakati inayotekelezwa na Halmashauri ya Jiji la Dodoma.
Alisema kuwa wamevutiwa na kiwango cha uwekezaji pamoja na
usimamizi madhubuti miradi hiyo na kubainisha kuwa Ilemela inakwenda kutumia
uzoefu huo kama darasa. Tunaipongeza Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwa kumiliki
na kuendesha miradi mikubwa na yenye tija kama hii. Sisi pia tuna miradi
inayofanana na hii. Hivyo, ziara hii imetupa nafasi ya kujifunza mambo mengi
ambayo tunaenda kuyafanyia kazi Ilemela ili tuweze kuboresha huduma na kuongeza
mapato yetu ya ndani kupitia miradi ya kimkakati” alisema Abdallah.
Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa
ya Ilemela, Samson Medda alisema kuwa ushirikiano na kubadilishana uzoefu kati
ya halmashauri ni njia muhimu ya kuharakisha maendeleo ya kiuchumi na kuboresha
utendaji wa taasisi za serikali za mitaa. “Tumekuja kujifunza na kuona kwa
vitendo namna ambavyo Jiji la Dodoma limefanikiwa kuwekeza katika miradi yenye
tija kwa wananchi. Maarifa na uzoefu tulioupata hapa utatusaidia kwenda
kuongeza ubunifu, ufanisi na usimamizi bora wa miradi yetu ya maendeleo Ilemela” alisema Medda.
Nae Diwani wa Viti Maalumu kupitia Chama cha ACT Wazalendo,
Neema Tambi alisema kuwa ziara hiyo iliongeza uelewa mkubwa kuhusu umuhimu wa
miradi ya kimkakati katika kukuza uchumi wa halmashauri. “Ziara hii imekuwa na manufaa makubwa
kwetu kwasababu tumepata ujuzi na uzoefu ambao tutakwenda kuufanyia kazi
Ilemela. Tukisimamia vizuri miradi ya kimkakati, tutaimarisha huduma kwa
wananchi na kuongeza mapato ya ndani ya halmashauri yetu” alisema Tambi.
Ziara ya mafunzo ya Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela katika
Jiji la Dodoma ikiangazia miradi ya hoteli, jengo la Kitega Uchumi Mtumba,
Bustani ya Mapumziko Chinangali na Soko la wazi la Machinga inajenga taswira
chanya ya ushirikiano baina ya mamlaka za serikali za mitaa hapa nchini, huku
ikionesha dhamira ya dhati ya viongozi hao katika kuhakikisha rasilimali za
umma zinatumika kwa ufanisi mkubwa ili kuleta maendeleo endelevu.
MWISHO
Comments
Post a Comment