Baraza la Biashara la Wilaya ya Dodoma lapongezwa kwa kuimarisha mazingira ya uwekezaji
Na. Mwandishi Wetu, DODOMA
Sekta ya Biashara na Uwekezaji Wilaya ya
Dodoma imepongezwa kwa kuboresha mazingira ya ufanyaji wa shughuli za kiuchumi,
hatua iliyochochea ongezeko la wafanyabiashara na wawekezaji wanaotumia fursa
zilizopo kukuza uchumi wa wilaya hiyo.
Hayo yalielezwa na Mwenyekiti wa Baraza la Biashara la Wilaya ya Dodoma, Alhaj Jabir Shekimweri alipokuwa akizungumza wakati wa Kikao cha Baraza la Biashara la Wilaya ya Dodoma kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Halmashauri jijini Dodoma.
Alilipongeza baraza hilo kwa kazi nzuri
wanayoendelea kuifanya katika kuhamasisha uwekezaji na shughuli za kiuchumi.
“Jiji letu limeendelea kusimamia mifumo inayotoa huduma kwa wananchi.
Tunaelezwa kuwa pale SGR huduma ya ‘shuttle’ inapatikana ambapo zinapunguza
kadhia kwa wageni ambao hawaujui usafiri wa bajaj na bodaboda. Pia Kanda
zimeanzishwa na zinafanya vizuri sana kwa kusaidia wananchi kupata huduma
zinazopatikana katika ofisi kuu, hali inayowasaidia kuepuka kupoteza muda na
gharama zisizo za lazima. Hapa leo tunawazungumzia wafanyabiashara wakubwa na
wawekezaji ambao ndio tunataka baraza hili liwasimamie ili mazingira ya
upatikanaji huduma uwe rafiki na hatimae tunafahamu utasisimua uchumi wa jiji
letu” alisema Alhaj Shekimweri.
Kwa upande wake, Katibu wa Baraza la
Biashara la Wilaya ya Dodoma, Dkt. Frederick Sagamiko alisema kuwa uanzishwaji
wa One Stop Business Centre ulikuwa mahsusi kwa ajili ya kuwahudumia wafanyabiashara
kwa urahisi zaidi. Aliongeza kuwa ni muhimu Jiji la Dodoma kupewa nafasi ya
uratibu pekee wa kituo hicho huku wafanyabiashara wakisimamia moja kwa moja
masuala yao, hatua itakayoongeza ufanisi na uwajibikaji.
Naye mjumbe kutoka sekta binafsi
anayewakilisha Chemba ya Kitaifa ya Wafanyabiashara Tanzania (TNCC), Idd Senge
alisisitiza umuhimu wa baraza hilo kuendelea kuwahamasisha wafanyabiashara na
wawekezaji kukutana mara kwa mara ili kujadili changamoto na fursa zilizopo.
Alisema hatua hiyo itasaidia kuhakikisha huduma zote muhimu zinazohitajika
zinapatikana kwa wakati na kuifanya Dodoma kuwa na mazingira rafiki ya biashara
na uwekezaji.
Comments
Post a Comment