Kampeni ya upandaji miti Jiji la Dodoma yafanikiwa S/M Mbwanga
Na. Mwandishi Wetu, DODOMA
Jiji la Dodoma limeendelea kutekeleza
kampeni ya upandaji miti ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuhifadhi mazingira na
kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi. Zoezi hilo limefanyika katika
maeneo mbalimbali ya jiji ikiwemo shule, taasisi za umma, barabara na maeneo ya
makazi.
Akizungumza katika Shule ya Msingi Mbwanga, Katibu Tawala wa Wilaya ya Dodoma, Sakina Mbugi alisema kuwa zoezi la upandaji miti ni muendelezo wa kulifanya Jiji la Dodoma kuwa la kijani na pia kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika siku yake ya kuzaliwa.
Aliwataka wanafunzi, walimu na wananchi kwa
ujumla kujenga utamaduni wa kupanda na kutunza miti ili kulinda mazingira na
kuhakikisha ustawi wa vizazi vijavyo. Alisisitiza kuwa upandaji wa miti shuleni
una mchango mkubwa katika kuelimisha watoto kuhusu umuhimu wa mazingira tangu
wakiwa wadogo. "Tunapanda miti hii kwasababu ya kuungana na Mhe. Rais,
Dkt. Samia kumpongeza katika siku yake ya kuzaliwa, ardhi hii itatunzwa na kuwa
imara kama mtaungana katika usimamizi mzuri wa miti tuliyopanda leo. Tunayo
Dodoma moja na inatutegemea sisi, kumbukeni jambo tulilofanya leo ni muhimu
sana kwasababu miti hii itatufaidisha sisi wenyewe. Pia itasaidia kuondokana na
mabadiliko ya tabianchi ikiwemo mafuriko na mmomonyoko wa ardhi" alisema
Mbugi.
Kwa upande wake Diwani wa Kata ya Mnadani,
Mugendi Kerenge, aliwataka wananchi kuendelea kushiriki kikamilifu katika
uhifadhi wa mazingira kwa kupanda na kutunza miti. Alisema kuwa wananchi
wanapaswa kuhifadhi vyanzo vya maji kwa kuwa ni jukumu la kila mmoja na sio
serikali pekee. “Ni muhimu kupanda miti na ni wajibu kuitunza hadi ikue. Hii
italinda ardhi yetu, kuleta mvua za uhakika na kuboresha maisha ya vizazi
vijavyo” alisema Kerenge.
Zoezi hilo lilishirikisha viongozi wa
serikali ya mtaa, wanafunzi, na wanachi ambapo jumla ya miti 150 ilipandwa
shuleni hapo. Wadau wote walioshiriki waendelee kuhakikisha kuwa zoezi la
upandaji miti linafanyika mara kwa mara ili Dodoma ibadilike kimazingira kwa
miaka ijayo.
Comments
Post a Comment