MADIWANI JIJI LA DODOMA WATAKIWA KUTATUA KERO ZA WANANCHI
Na. Mwandishi Wetu, DODOMA
Madiwani
wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma watakiwa kusikiliza kero za wananchi na
kuhakikisha zinapatiwa ufumbuzi kwa wakati ili kuimarisha maendeleo na ustawi
wa jamii.
Hayo aliyasema Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Alhaji Jabir Shekimweri, wakati alipokuwa akizungumza katika Mkutano wa Baraza la Madiwani uliofanyika katika ukumbi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma.
Alisema
kuwa madiwani ni kiungo muhimu kati ya serikali na wananchi, hivyo wanapaswa
kuwa mstari wa mbele katika kushughulikia changamoto zinazowakabili wananchi
katika maeneo yao. “Madiwani ni sauti ya wananchi. Ni muhimu msikilize kwa
umakini kero zao na kuzitatua kwa wakati ili kuondoa malalamiko yasiyo ya
lazima na kuongeza imani ya wananchi kwa serikali yao” alisema Alhaji Shekimweri.
Aliongeza
kuwa utekelezaji wa majukumu hayo unahitaji uwajibikaji, ushirikiano na
ufuatiliaji wa karibu wa miradi ya maendeleo ili kuhakikisha inaleta matokeo
yaliyokusudiwa.
Kwa
upande wake, Diwani wa Kata ya Makole, Omary Omary, alisema kuwa madiwani
wanaendelea kuchukua hatua madhubuti katika kusikiliza na kutatua changamoto za
wananchi pamoja na kusimamia miradi ya maendeleo inayotekelezwa katika kata
zao. “Sisi madiwani tupo karibu na wananchi wetu kila wakati. Tumejipanga
kuhakikisha tunasikiliza kero zao na kuzitafutia ufumbuzi kwa kushirikiana na
wataalamu pamoja na kusimamia ipasavyo miradi yote ya maendeleo,” alisema
Omary.
Mkutano huo wa Baraza la Madiwani umeendelea kuwa jukwaa muhimu la kujadili na kuweka mikakati ya kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi, huku viongozi wakihimizwa kuzingatia uwajibikaji na ushirikiano katika kuleta maendeleo endelevu katika Jiji la Dodoma.
Comments
Post a Comment