Jiji la Dodoma lajipanga kung’ara kwa usafi, Bilioni tatu yatengwa kwaajili ya miundombinu ya taka

Na. Mwandishi Wetu, DODOMA

Halmashauri ya Jiji la Dodoma imeendelea kuonesha dhamira ya dhati ya kuboresha mazingira na afya za wakazi wake baada ya kuweka mpango mkakati wa kutenga shilingi bilioni tatu katika bajeti mpya ya fedha ijayo kwa ajili ya kuimarisha miundombinu ya ukusanyaji wa taka.


Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake kuhusu mpango huo, Mstahiki Meya wa Jiji la Dodoma, Alimwoni Chaula alisema kuwa bajeti hiyo inalenga kulifanya Jiji la Dodoma kuwa miongoni mwa majiji safi nchini kwa kuweka mifumo rafiki na ya kisasa ya kushughulikia taka.

Alieleza kuwa fedha hizo zinatokana na mapato ya ndani, jambo linaloonesha uwezo wa jiji kujitegemea katika kugharamia miradi ya maendeleo. “Suala la usafi wa mazingira halikwepeki na sisi tunasema kuwa haitawezekana kuwa na jiji chafu. Kwenye bajeti yetu mpya tumetenga takribani shilingi bilioni tatu kwaajili ya kuhakikisha vifaa vyote vya kukusanyia taka vinapatikana” alisema Chaula.

Katika utekelezaji wake, jiji linatarajia kusambaza madastbini makubwa katika maeneo mbalimbali, yatakayokuwa na mfumo wa utenganishaji wa taka. Hatua hiyo itarahisisha ukusanyaji, usafirishaji na uchakataji wa taka, huku ikilenga pia kulinda mazingira na kupunguza athari za kiafya kwa wananchi. “Mkakati wetu ni kuhakikisha Jiji letu linakuwa safi muda wote. Hili linawezekana kwa kuweka miundombinu bora na kwa kushirikiana na wananchi” alisisitiza Chaula.

Aidha, aliwataka wananchi kuendelea kulipa kodi kwa wakati ili kuwezesha utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo usafi wa jiji, huku akiongeza kuwa mchango wa wananchi kupitia kodi ndio msingi wa maboresho ya huduma wanazozipata kila siku.

Mpango huo unatarajiwa kuleta mageuzi makubwa katika usimamizi wa taka, kulifanya jiji kuwa na mandhari safi, salama na linalovutia zaidi kwa wakazi na wageni.

MWISHO

 

Comments

Popular Posts

Wananchi waitwa kupima magonjwa yasiyoambukiza bure Nyerere Square

TAMISEMI yakusanya Shilingi Trilioni 1.11

Ukarabati Shule ya Msingi Iyumbu kupunguza msongamano darasani