Wananchi washirikishwe katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo
Na. Dennis Gondwe, DODOMA
NAIBU
Meya wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Fadhili Chibago ametoa rai kuwa miradi
yote ya maendeleo inayotekelezwa wananchi washirikishwe kikamilifu ili wawe sehemu
ya miradi hiyo na kusema kuwa utaratibu huo utaifanya miradi kudumu kwa muda
mrefu.
Kauli hiyo aliitoa alipoongoza Kamati ya Fedha na Utawala timu namba tatu kutembelea na kukagua umaliziaji wa vyumba vitatu vya madarasa katika Shule ya Msingi Nguji iliyopo Kata ya Ng’hong’onha, jijini Dodoma.
Alisema
kuwa halmashauri inatekeleza miradi mingi ya maendeleo. “Nitumie nafasi hii
kuwasisitiza kuendelea kuwashirikisha wananchi wa eneo husika kwenye
utekelezaji wa miradi ya maendeleo. Wananchi wakishirikishwa wanakuwa wamiliki
wa mradi husika. Wasiposhirikishwa wanajiona siyo sehemu ya mradi. Hata kama
kuna mtu anataka kufanya uharibifu kwenye mradi, wananchi wanabaki wanamtazama
kwa sababu hawajashirikishwa. Nitumie nafasi hii kutoa rai, kwenye miradi yetu
tunapoitekeleza, tuwashirikishe wananchi kuanzia mwanzo wa mradi hadi
utakapokamilika ili wao waone fedha wanazolipa kama kodi zinavyofanya kazi.
Vilevile, niwashukuru wadau mbalimbali wanaosaidia kutoa fedha kuhakikisha
miradi yetu inakamilika kwa wakati” alisema Chibago.
Shule ya Msingi Nguji ilipelekewa shilingi 21,000,000 kwa ajilia ya umaliziaji vyumba vitatu vya madarasa, ujenzi wa Ofisi ya Machinga Mkoa ilipelekewa shilingi 52,460,000 na ukamilishaji wa miundombinu na ujenzi wa mabweni mawili, vyumba vinne vya madarasa, matundu 10 ya vyoo na nyumba pacha ya walimu Shule ya Sekondari Miyuji B ilipelekewa shilingi 567,000,000.
MWISHO
Comments
Post a Comment