Shule mpya ya Kata, Sekondari Miyuji B yajengwa kisasa kutoa elimu bora

Na. Dennis Gondwe, DODOMA

KAMATI ya Fedha na Utawala ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma imempongeza Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa nia yake njema ya kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora hasa za elimu baada ya kutembelea na kukagua miradi ya maendeleo yenye zaidi ya shilingi 500,000,000 katika kata tatu za jiji hilo.




Kauli hiyo ilitolewa na Naibu Meya wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Fadhili Chibago alipoongoza timu namba tatu ya Kamati ya Fedha na Utawala kutembelea na kukagua miradi ya maendeleo katika kipindi cha robo ya tatu ya Mwaka wa Fedha 2024/2025.

Alisema kuwa kamati yake ilitembelea kata tatu za Ng’hong’ohna, Makole na Miyuji kukagua miradi ya maendeleo. “Leo tumekuwa na ziara nzuri ya kutembelea miradi mbalimbali katika kata tatu za Halmashauri ya Jiji la Dodoma. Kamati ya Fedha na Utawala tuligawana na kupeana majukumu ya kutembelea miradi ya maendeleo. Timu yangu tumekagua umaliziaji wa vyumba vitatu vya madarasa Shule ya Msingi Nguji, Kata ya Ng’hong’onha, ujenzi wa Ofisi ya Machinga Mkoa wa Dodoma na ukamilishaji wa miundombinu Shule ya Sekondari Miyuji B ulipo ujenzi wa mabweni mawili, vyumba vinne vya madarasa, matundu 10 ya vyoo na nyumba pacha ya walimu” alisema Naibu Meya Chibago.

Akiongelea utekelezaji wa miradi hiyo alisema kuwa imetekelezwa kwa kiwango bora. “Kamati tumejiridhisha kwamba fedha za serikali na walipa kodi zimetumika kwa usahihi. Miradi yote imejengwa kwa kuzingatia vigezo vyote vinavyohitajika na ubora umezingatiwa. Kwa niaba ya Kamati ya Fedha na Utawala ya Jiji la Dodoma, nimshukuru sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan katika nia yake njema ya kuhakikisha wananchi wa Dodoma wanafikiwa na huduma zilizo bora. Watoto wetu wasome katika madarasa mazuri, lakini pia wapate huduma nzuri kutoka kwa walimu wao. Sisi Kamati ya Fedha na Utawala tutaendelea kumuunga mkono katika kutekeleza majukumu yake” alisema Naibu Meya Chibago.   



Akisoma taarifa ya ujenzi wa Shule ya Sekondari Miyuji B kwa Kamati ya Fedha na Utawala, Mkuu wa Shule hiyo, Mwl. Clara Mwinshehe alisema kuwa shule yake ilianza mwaka 2024 kutokana na fedha za Mradi wa Kuimarisha Elimu ya Sekondari (SEQUIP).  “Shule ilipokea shilingi 454,000,000 mwaka wa fedha 2023/2024 kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu. Nyumba pacha ya walimu shilingi 95,000,000, mabweni mawili shilingi 250,000,000, matundu 10 ya vyoo shilingi 17,000,000 na madarasa manne shilingi 92,000,000. Kati ya fedha hizo kiasi kilichotumika ni shilingi 340,000,000 na malipo mengine yapo kwenye utaratibu” alisema Mwl. Mwinshehe.

Katika shule hiyohiyo, Halmashauri ya Jiji la Dodoma ilitoa kiasi cha shilingi 113,000,000 fedha kutoka mapato ya ndani kwa ajili ya umaliziaji na ukarabati ya jengo la TEHAMA, maktaba, madarasa matatu, choo matundu 10, maabara tatu za Fizikia, Kemia na Baiolojia pamoja na gharama ya kuunganisha umeme kwenye majengo yote.

Shule ya Sekondari Miyuji B ni shule ya kata iliyoanzishwa mwaka 2024, ina wanafunzi 208, wanafunzi wa Kadato cha Pili 163 na Kidato cha Kwanza walioripoti ni 80.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Jiji la Dodoma lapewa angalizo lishe bora kwa wananchi

RC Dodoma apongeza wafugaji kwa ushiriki wa Paredi ya Mifugo

Vijana waalikwa kushiriki Kongamano S/M Mbwanga