Jengo jumuishi la kutolea huduma za Afya Makole lipo katika hatua nzuri ya ujenzi

Na. Nancy Kivuyo, MAKOLE

Mradi wa ujenzi wa jengo jumuishi la kutolea huduma za afya katika Kituo cha Afya Makole wenye zaidi ya shilingi bilioni moja lipo katika hatua nzuri ya utekelezaji wake.




Kauli hiyo ilitolewa na Kaimu Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya Makole, Dkt. Salma Gwassa alipokuwa akisoma taarifa ya mradi wa ujenzi wa Kituo cha Afya Makole kwa Kamati ya Fedha na Utawala ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma iliyotembelea maendeleo ya mradi huo.

Alisema kuwa kiasi cha shilingi 750,000,000 kimetolewa na serikali kuu na fedha za mapato ya ndani ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma shilingi 289,794,329 zimelipwa kwa mkandarasi kwaajili ya ujenzi huo.

Alisema kuwa ujenzi upo katika hatua ya msingi na wanatarajia mradi utakapokamilika wananchi wa Kata ya Viwandani na Jiji la Dodoma kwa ujumla watapata matibabu hapo. “Mradi huu ukikamilika huduma za kliniki za kibingwa ‘speciality clinic’ zitapatikana, huduma za kiutawala zitaboreka na tutapanua wigo wa utoaji wa huduma kwa wagonjwa wa nje na wa ndani” alisema Dkt. Gwassa.




Nae, Msimamizi wa mradi, Mhandisi Ntezimana Chongele alisema kuwa mradi upo katika hatua nzuri na utatekelezeka kwa wakati. “Napenda kuwahakikishia kuwa mkandarasi yupo vizuri, eneo hili lina asili ya maji kama mnavyoona amefanya kazi kubwa kuyavuta na anatarajia kuendelea na ujenzi kwa kasi kuhakikisha anamaliza mradi ndani ya muda uliopangwa” alisema Mhandisi Chongele.

Kwa upande mwingine Mwenyekiti wa Kamati ya Uchumi, Elimu na Afya Jiji la Dodoma, Joan Mazanda aliisisitiza kamati ya mradi kusimamia vizuri mradi huo ili ukamilike kwa wakati wananchi wapate huduma za matibabu. “Kituo cha Afya Makole kinatoa huduma za afya nzuri sana, tunategemea ujenzi ukikamilika wananchi watapata huduma nzuri. Nawasisitiza kusimamia vilivyo mradi huu, fedha iliyotolewa ni nyingi tutafurahi kuona unakamilika kwa viwango vile tunavyotarajia” alisisitiza Mazanda.




Mradi wa ujenzi wa jengo jumuishi la kutolea huduma za afya Kituo cha Afya Makole unatarajiwa kukamilika tarehe 27 Januari, 2026 na unatarajia kuhudumia wananchi 95,320 kwa mwaka. 

MWISHO

Comments

Popular Posts

Osterbay Dodoma wajitokeza usafi wa mazingira

Usafi wa Mazingira Kipaumbele Kata ya Chamwino

Wananchi wa Kata ya Mtumba wanufaika na Mikopo ya asilimia 10 ya Halmashauri