Ujenzi wa Darasa Sekondari Anthony Mavunde kupunguza msongamano kwa wanafunzi

Na. Nancy Kivuyo, HOMBOLO BWAWANI

Mkuu wa Shule ya Sekondari Anthony Mavunde, Mwalimu Emmanuel Magumba amesema kuwa shule hiyo ilipokea kiasi cha shilingi 15,425,000 kwa ajili ya ujenzi wa darasa moja na ununuzi wa viti 50 na meza 50 kwa lengo la kuongeza miundombinu katika shule hiyo.



Mwl. Magumba alisoma taarifa ya mradi huo mbele ya Kamati ya Fedha na Utawala ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma na kusema kuwa pamoja na ujenzi unaoendelea anaiomba halmashauri iwaongezee fedha kwa ajili ya kumalizia darasa hilo. “Hatua tuliyofikia ni nzuri kwasababu umaliziaji darasa hili sio mkubwa kama unavyoanza ujenzi” alisema Mwl. Magumba.

Aliongeza kuwa kukamilika kwa darasa hilo kutaleta chachu ya wanafunzi kusoma kwa bidii. “Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa ujenzi wa darasa hili ukikamilika naamini wanafunzi wetu watapata nafasi ya kusoma na wataongeza bidii katika masomo” aliongeza Mwl. Magumba.



Nae, Mwanafunzi wa Kidato cha Kwanza, Emmanuel Mbega alisema kuwa anaishukuru serikali kwa kuwajengea shule karibu. “Napenda kutoa shukrani kwa serikali kwa kutujali sisi wanafunzi. Kiukweli uwepo wa Sekondari ya Anthony Mavunde umetupunguzia adha ya kwenda mbali kusoma” alishukuru Mbega.

Kwa upande mwingine Mwanafunzi wa Kidato cha Pili, Salma Malima alisema kuwa uwepo wa sekondari hiyo umeondoa adha ya kutembea umbali wa kilomita nane kufuata shule Hombolo. ”Tunashukuru sana kuwepo shule hii hapa, kwanza imetusaidia kupunguza umbali wa kutembea kwenda shuleni. Lakini imetusaidia sisi wanafunzi wa kike kuepukana na vishawishi vya barabarani. Wapo wenzetu walipata mimba za utotoni sababu ya mazingira magumu ya kufika shuleni. Nina furaha sana kusoma hapa sasa” alishukuru Malima.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Jiji la Dodoma lapewa angalizo lishe bora kwa wananchi

RC Dodoma apongeza wafugaji kwa ushiriki wa Paredi ya Mifugo

Rais Samia: Tumieni kikamilifu Miundombinu, Teknolojia na mitaji iliyowekezwa katika Kilimo, Uvuvi na Mifugo