Baraza la Madiwani la Jiji la Dodoma lapitisha Hesabu za Mwaka 2023/2024

Na. Valeria Adam, DODOMA

Baraza la Madiwani la Jiji la Dodoma limefunga rasmi hesabu za mwaka wa fedha unaoishia tarehe 30 Juni 2024, baada ya kupokea, kujadili na kupitisha taarifa ya ufungaji wa hesabu za halmashauri.




Kwa mujibu wa Mweka Hazina wa Halmashauri ya Jiji, CPA. David Rubibira alisema chanzo kikuu cha mapato ya halmashauri hiyo ni tozo, faini na ushuru mbalimbali. Mapato mengine yanatokana na michango ya afya, uwekezaji, pamoja na ruzuku kutoka Serikali Kuu, aliongeza.

"Mapato na matumizi ya ndani ya halmashauri ni pamoja na mapato yenye tozo (kodi) ambayo ni kiasi cha shilingi bilioni 34.7, faini na tozo ni shilingi bilioni 2.6, Mapato mengineyo ni shilingi bilioni 6.6. Michango mengineyo ya afya ni shilingi bilioni 1.9, mapato yapatikanayo kwenye uwekezaji ni shilingi bilioni 5.5 na mapato toka serikali kuu ni shilingi bilioni 83.08 ambapo jumla ya mapato na matumizi yote ya ndani ya halmashauri ni shilingi bilioni 134.4" alisema CPA. Rubibira.

Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Chang'ombe, Bakari Fundikira alisisitiza kuwa taarifa hiyo ni muhimu katika kutoa mwelekeo wa utekelezaji wa shughuli za halmashauri kwa mwaka ujao wa fedha.

Alibainisha kwamba, kuweka mambo sawa katika shughuli za halmashauri itawasaidia kujiandaa vyema kwa ajili ya ukaguzi wa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali.

Fundikira alieleza kuwa baraza linapaswa kuhakikisha kuwa hakuna mapungufu yanayoweza kuathiri tathmini ya utendaji wa halmashauri.

"Taarifa hii itupe dira ya utekelezaji wa shughuli zetu zote za halmashauri katika kuhakikisha tunaweka mambo sawa. Hata Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali atakapokuja, basi mambo mengine tuwe tumeyaweka sawa tayari," alisema Fundikira akihitimisha mchango wake kwenye mkutano huo.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma