Barabara ya Dodoma Makulu – Ntyuka kuboresha maisha ya wananchi
Na. Abdul Juma, DODOMA MAKULU
Ujenzi wa Barabara ya kilometa 5.2 inayounganisha Kata ya Dodoma Makulu na
Ntyuka kutatua changamoto ya usafi kwa kata hizo na kufanya maisha ya wananchi
kuwa bora.
Kauli hiyo ilitolewa na Mwenyekiti wa Mtaa wa Msangalale
Magharibi Kata ya Dodoma Makulu, Leonard Ndama alipokuwa akiongelea mchango wa
Barabara ya lami yenye urefu wa kilometa 5.2 katika mafanikio ya serikali ya
awamu ya sita kwa kipindi cha miaka minne.
Alisema kuwa serikali ya awamu ya sita chini ya Rais, Dkt
Samia Suluhu Hassan kwa kipindi cha miaka minne ilianza ujenzi wa barabara
yenye kiwango cha lami iliyokuwa ni changamoto kwa wakazi wa Kata ya Dodoma
Makulu walipotaka kwenda Ntyuka kufuata huduma za kijamii. Alisema kuwa
walikuwa wakitumia muda mrefu njiani na kuchelewa shughuli zao jambo
lililosababisha uchumi wao kuwa chini.
“Tumepata mradi huu wa barabara inayotoka Dodoma Makulu
kwenda Ntyuka ambayo imeleta manufaa ya kibiashara hata katika usafiri kwasababu
wananchi wamekuwa wakitumia barabara hii. Naomba wananchi wa Dodoma Makulu
tuitunze miundombinu hii tuliyojengewa na serikali ili tuweze kurithisha vizazi
vyetu vijavyo” alisema Ndama.
Nae, mwananchi wa Kata ya Dodoma Makulu, Nazarius Moshi anayejishughulisha
na biashara ya usafirishaji maarufu kama bodaboda, alieleza namna barabara hiyo
itakavyoleta faida kwa watumiaji wa barabara hiyo itakapo kamilika hasa wafanya
biashara ya usafirishaji (bodaboda). “Barabara hii ikikamilika itakuwa na faida
kwetu kwasababu kwanza, itaturahisishia katika shughuli zetu za usafirishaji wa
abiria kutoka Kata ya Ntyuka, zamani tulikuwa tunateseka sana na ubovu wa
barabara hii. Pili, itarahisisha wananchi kuzifikia huduma za kijamii nje ya
kata hii kwa urahisi” alisema Moshi.
MWISHO
Comments
Post a Comment