Jiji la Dodoma kuanza ujenzi wa Jengo Jumuishi Kituo cha Afya Makole
Na. Faraja Mbise, MAKOLE
Halmashauri ya Jiji la Dodoma inatarajia kuanza ujenzi
wa Jengo Jumuishi katika Kituo cha Afya Makole ambao unatarajiwa kuanza tarehe
27 Januari, 2025 chini ya Mkandarasi Mohanmmedi Builders Limited.
Akizungumzia kuhusu huduma zitakazokuwa zinapatikana
katika jengo hilo jumuishi Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya Makole, Dkt.
Revocatus Baltazary alisema zitapatikana huduma mbalimbali kwa ajili ya kukidhi
huduma zote za kiafya. “Jengo hili linaenda kujibu yote hayo, kwasababu huduma
zitakazoenda kupatikana ni huduma za ‘emergency’, radiolojia, maabara, vyumba
vya madaktari vitaongezwa. Pia kuna wodi za kulaza watoto chini ya umri wa
miaka mitano, magonjwa ya ndani kwa wanawake na wanaume. Vilevile, wodi za
upasuaji na ‘floor’ ya wakina mama wajawazito” alisema Dkt. Baltazary.
Sambamba na hilo, alisema kuwa lengo hasa la kujenga jengo
hilo ni kukosekana kwa baadhi ya huduma kama ‘emergency’, huduma za kulaza, na jengo
la upasua. “Jengo hili linajengwa kutokana na baadhi ya huduma zinazokosekana
katika Kituo cha Afya Makole ikiwepo huduma za ‘emergency’, huduma za kulaza,
lakini pia ‘theatre’ ipo moja na pia wodi za upasuaji. Kwahiyo, jengo hili
linaenda kujibu yote hayo”.
Kwa upande wake Mhandisi wa Jiji, Nicodemus Kileo, alisema
kuwa wanatarajia utekelezaji wa mkataba wa ujenzi huo utakamilika ndani ya
wakati uliopangwa. Pia alimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa
ajili ya kutoa fedha ya ujenzi wa vituo vya Afya. “Ni matarajio yetu kwamba,
utekelezaji wake utaenda ‘smooth’ na utakamilika ndani ya ule muda uliopangwa
na tunategemea usizidi. Tunamshukuru Mheshimiwa Rais kwa fedha ambazo
zimetolewa ikiwa na lengo la kukidhi haja na mahitaji ya mji inayopelekea kuwa
na changamoto kubwa ya masuala ya kiafya” alisema Mhandisi Kileo.
Nae, Mkandarasi kutoka Mohammedi Builders Limited, Meneja
Mohammed Jafferji, alisema kuwa, anategemea kukamilisha ujenzi wa mradi huo
kabla ya muda uliopangwa. “Tunategemea kuanza ujenzi kuanzia Jumatatu tarehe 27
Januari, 2025 na itatuchukua mwaka mmoja kukamilisha mradi huo kama ‘contract’
inavyosema. Lakini tutajitahidi kukamilisha na kuumaliza kabla ya wakati
uliopangwa” alisema Meneja Jafferji.
Mradi wa ujenzi wa Jengo Jumuishi Kituo cha Afya
Makole unasimamiwa na Mkandarasi Mohammedi Builders Limited, ambapo
amekabidhiwa eneo siku ya tarehe 24 Januari, 2025. Mkataba huo ulisainiwa
tarehe 17 Januari, 2025 na utadumu kwa muda wa miezi kumi na miwili.
MWISHO
Comments
Post a Comment