Wakuu wa Shule Jiji la Dodoma wapewa mafunzo ya mfumo wa NeST

 Na. Coletha Charles, DODOMA

Wakuu wa Shule za Sekondari Halmashauri ya Jiji la Dodoma wamewezeshwa mafunzo ya ununuzi kwa njia ya mtandao serikalini ‘National e-Procurement System of Tanzania’ (NeST) yatakayoboresha utendaji kazi na kuwawezesha kupata mafundi na watoa huduma kupitia mfumo wa manunuzi.




Mafunzo hayo yalitolewa na Kitengo cha Manunuzi na Ugavi kwa lengo la kuongeza ufanisi na uwazi kwa kufanya shughuli za ununuzi kutokana na mabadiliko ya Sheria ya Mwaka 2023 na Kanuni za Manunuzi za Mwaka 2024, katika ukumbi wa Shule ya Sekondari Umonga.

Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma, Afisa Elimu Vifaa na Takwimu, Fredrick Mwakisambwe, alifafanua mfumo wa manunuzi kwa njia ya kielektroniki, ni mfumo ambao unarahisisha mchakato wa manunuzi na kuleta ufanisi mkubwa katika utendaji kazi.

Alisema kuwa mafunzo hayo ni mahususi kwa wakuu wa shule wakiambatana na walimu wanaohusika kuratibu na kusimamia fedha ambazo zinapelekwa katika shule za sekondari kwa kuelekezwa namna sahihi ya kutumia mfumo mpya wa manunuzi ambao ni NeST’. “Ufanisi kwa mwaka 2025 utakuwa mkubwa hasa katika manunuzi ya vitu mbalimbali vya shule za sekondari. Kwahiyo, mfumo huu tumeona jinsi ambavyo ulivyokuwa mzuri na huru, ukilinganisha na utaratibu wa zamani ambao ulikuwa siyo wa mfumo na ulikuwa unapelekea wakati mwingine udanganyifu au ukiukwaji mkubwa wa taratibu za manunuzi. Tunatarajia baada ya mafunzo haya walimu wetu watakuwa na uelewa wa kutosha katika matumizi ya manunuzi ya vifaa kwa kutumia fedha za serikali” alisema Mwakisambwe.

Nae, Muwezeshaji wa mafunzo hayo, Afisa Manunuzi kutoka Kitengo cha Manunuzi na Ugavi, Mary Ngailo, alieleza kuwa mfumo mpya wa manunuzi, ‘NeST,’ utaongeza uwazi na ufanisi katika michakato ya ununuzi serikalini kwa kupunguza gharama na muda unaotumika katika taratibu za manunuzi kwa kuleta tija kwa taasisi za umma.



Alisema kuwa mfumo huu utasaidia taasisi nyingi za umma kuboresha ufanisi wa taratibu za manunuzi ‘NeST’, ambao ni jukwaa la kidijitali na kuwezesha uratibu wa zabuni na ununuzi kwa kutumia teknolojia ya kisasa. “Sheria imeitaka taasisi husika kutumia njia ya kielektroniki kufanya manunuzi. Kwahiyo, mwalimu na mzabuni hawaonani ana kwa ana mwalimu atatuma mapendekezo yake au mahitaji yake kwenye mfumo na mzabuni atakaye kidhi vigezo ataomba. Lakini kumekuwa na changamoto ya bei inayoombwa na mzabuni unakuta ipo juu kuliko bei ambayo inakuwa imekadiliwa kuwa ni bei ya soko, baada ya kutokea shida kama hiyo inafanyika ‘negotiation,’ na kwa sasa sheria imekuja kukataza matumizi ya kufanya ‘negotiation’ kwa kutumia simu na badala yake inataka majadiliano yafanywe na timu ya majadiliano ambayo itateuliwa na afisa masuhuli wa taasisi husika” alisema Ngailo.

Kwa upande wake, Mkuu wa Shule ya Sekondari Mbabala, Mwl. Patrick Mayengo, alionesha furaha yake baada ya wakuu wa shule kupata mafunzo ya mfumo mpya wa manunuzi wa ‘NeST’. Alisema kuwa mfumo huo utaleta mapinduzi katika ufanisi wa ununuzi na usimamizi wa rasilimali shuleni.

Alisema kuwa mfumo wa ‘NeST’ utasaidia kuboresha utoaji wa huduma kwa walimu kwa kuhakikisha kuwa vifaa vya shule vinanunuliwa kwa haraka, kwa usahihi na kwa gharama nafuu. “Mfumo huu utakuwa suluhisho la kudumu, kwasababu unahakikisha usalama na uwazi katika manunuzi yote. Mfumo huu unatusaidia kutangaza zabuni ambazo mtu anakutana nazo huko kwenye mfumo siyo mpaka nimtafute ‘physically” alisema Mwl. Mayengo.

MWISHO

 

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma