Shilingi Bil. 2.1 zatolewa kujenga miundombinu Sekta ya Afya
Na. Dennis Gondwe, DODOMA
WILAYA ya Dodoma imepokea shilingi 2,145,756,727.12 kwa
ajili ya ujenzi wa miundombinu na ununuzi wa samani na vifaa tiba katika
jitihada za serikali kuboresha huduma za afya wilayani hapa.
Kauli hiyo ilitolewa na Katibu Tawala Wilaya ya Dodoma,
Sakina Mbugi alipokuwa akisoma Risala ya Utii kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan wakati wa Mbio za Mwenge wa
Uhuru Wilaya ya Dodoma katika uwanja wa Shule ya Msingi Kizota jijini Dodoma.
Alisema kuwa katika
kipindi cha Mwaka wa Fedha 2025/2026 wilaya ilipokea kiasi cha
shilingi 2,145,756,727.12 kwa
ajili ya sekta ya afya. “Kati ya fedha hizo shilingi 1,945,756,727.12
ni kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu
ya afya na kiasi cha shilingi 200,000,000 ni kwa ajili ya ununuzi wa samani na vifaa tiba. Wilaya inakamilisha ujenzi
wa Hospitali ya Jiji, Kituo cha Afya Zuzu, Chang’ombe, Msalato, Zahanati ya
Kiwanja cha Ndege, Tambukareli na Jengo jumuishi Makole. Fedha hizi zimetoka
serikali kuu na Halmashauri ya Jiji” alisema Mbugi.
Mwenge wa Uhuru Mwaka 2026 unaongozwa na kaulimbiu
isemayo ‘Tanzania ni Yetu Sote,
Tushikamane kwa pamoja Kuleta Maendeleo ’.
MWISHO
Comments
Post a Comment