Viwanda 17 vya kurejesha Taka za Plastiki vyaanzishwa Wilaya ya Dodoma
Na. Dennis Gondwe, DODOMA
WILAYA ya Dodoma imefanikiwa kuanzisha viwanda 17 vya
kurejesha taka za plastiki na kugawa vifaa 12 vya kutenganisha na kuhifadhi
taka kwa lengo la kuweka mazingira safi na salama kwa shughuli na maisha
kuendelea.
Kauli hiyo ilitolewa na Katibu Tawala Wilaya ya Dodoma,
Sakina Mbugi alipokuwa akisoma Risala ya Utii kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan wakati wa Mbio za Mwenge wa
Uhuru Wilaya ya Dodoma katika uwanja wa Shule ya Msingi Kizota jijini Dodoma.
Alisema kuwa wilaya kwa
kushirikiana na wadau wa mazingira ilifanikiwa kuanzisha viwanda 17 vya
kurejeresha taka za plastiki, kugawa vifaa 12 vya kutenganisha na kuhifadhi
taka na elimu inaendelea kutolewa kwa wananchi, mashirika na taasisi katika
kudumisha utamaduni wa usafi na uhifadhi wa mazingira. “Mheshimiwa Rais, wilaya inakadiriwa kuzalisha wastani wa tani 458 za taka ngumu kwa siku, ambapo
wastani wa tani 305 sawa na
asilimia 66.5 hupelekwa kwenye Dampo la kisasa Chidaya lenye ukubwa wa ekari 48“ alisema Mbugi.
Akiongelea eneo la Nishati safi, alisema kuwa wilaya
inaendelea kuhakikisha wananchi wanahamia katika matumizi ya Nishati safi ya kupikia kwa kuhimiza
utumiaji wa mkaa poa na gesi. “Aidha, tayari taasisi 379 za umma na binafsi
zinazoandaa chakula cha watu wanaozidi
100 zimeacha matumizi ya mkaa na kuni ikiwa ni utekelezaji wa mikakati
kufikia Dira ya Matumizi ya Nishati Safi 2030. Pia, zaidi ya mitungi 2,800 imegawiwa kwa mama na baba lishe,
wanufaika wa mpango wa kunusuru kaya maskini na wajasiriamali kwenye kata“
alisema Mbugi.
Akiongelea sekta ya Maliasili, alisema kuwa kwa Mwaka
2025/2026, wilaya imefanikiwa kugawa, kuotesha na kustawisha miti 921,000 kwa kushirikiana na wadau mbalimbali na
zoezi hili ni endelevu. Wilaya imetoa elimu na kutundika mizinga 16 ya nyuki na
kuondoa makundi ya nyuki hatarishi kwa jamii, aliongeza.
MWISHO
Comments
Post a Comment