Mashine za Kieletroniki zakusanya Bil. 54.8 wilayani Dodoma
Na. Dennis Gondwe, DODOMA
WILAYA
ya Dodoma imekusanya shilingi 54,886,235,688.85 sawa na asilimia 76.6 ya lengo
la mwaka la kukusanya shilingi 71,675,239,000 kwa Mwaka wa Fedha 2025/2026 kwa
kutumia mashine za kieletroniki.
Kauli hiyo ilitolewa na Katibu Tawala Wilaya ya Dodoma,
Sakina Mbugi alipokuwa akisoma Risala ya Utii kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan wakati wa Mbio za Mwenge wa
Uhuru Wilaya ya Dodoma katika uwanja wa Shule ya Msingi Kizota jijini Dodoma.
Akiongelea ukusanyaji kodi na mapato kwa
mfumo wa TEHAMA, alisema kuwa wilaya inakusanya mapato ya serikali kupitia mfumo wa
TAUSI. ”Mheshimiwa Rais, katika
Mwaka wa Fedha 2023/2024 wilaya ilianza kutumia mfumo mpya uitwao TAUSI katika
ukusanyaji wa vyanzo vyote vya mapato. Kwa kipindi cha kuanzia Julai, 2025 hadi Aprili, 2026, wilaya imefanikiwa kukusanya
shilingi 54,886,235,688.85 sawa na
asilimia 76.6 ya lengo la shilingi
71,675,239,000 kwa mwaka kwa kutumia mashine za kielektroniki” alisema
Mbugi.
Kuhusu sekta ya biashara, alisema kuwa wilaya imefanikiwa
kusajili wafanyabiashara kwenye mfumo wa serikali za mitaa kwa ukusanyaji
mapato. ”Katika mwaka 2025/2026 wilaya imefanikiwa kutoa jumla ya leseni za biashara 17,521
ambazo zimeingiza shilingi 3,012,907,294 sawa na asilimia 76.6 ya lengo la
mwaka na leseni za vileo 1,201
ambazo zimeingiza shilingi 63,955,000
sawa na asilimia 74.3 ya lengo
la mwaka” alisema Mbugi.
Mwenge wa Uhuru Mwaka 2026 unaongozwa na kaulimbiu
isemayo ‘Tanzania ni Yetu Sote,
Tushikamane kwa pamoja Kuleta Maendeleo ’.
MWISHO
Comments
Post a Comment