Dodoma kuvuna Tani 40,930 Chakula na Nafaka
Na. Dennis Gondwe, DODOMA
WILAYA ya Dodoma inatarajia kuvuna tani 40,930 za mazao
ya chakula na biashara katika kuwahakikishia wananchi lishe bora na kujikwamua
kiuchumi.
Kauli hiyo ilitolewa na Katibu Tawala Wilaya ya Dodoma, Sakina Mbugi alipokuwa akisoma Risala ya Utii kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan wakati wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Wilaya ya Dodoma katika uwanja wa Shule ya Msingi Kizota jijini Dodoma.
Alisema kuwa wilaya kupitia Divisheni ya
Kilimo Mjini na wadau iliendelea kuhakikisha wananchi wanapata lishe bora na
kujikwamua kiuchumi kwa kulima mazao ya chakula na biashara. “Hali ya
upatikanaji wa chakula na bei ni ya wastani kwa msimu wa kilimo 2025/2026.
Wakulima wameanza kuvuna na kiasi cha tani 40,930 kinatarajiwa kuzalishwa. Hata hivyo, kuna mtiririko mzuri
wa mazao ya chakula yanayoingia na kupatikana katika masoko yote. Hivyo,
kuhakikisha upatikanaji wa chakula katika kipindi chote cha mwaka” alisema
Mbugi.
Akiongelea
sekta ya mifugo, alisema kuwa wilaya iliendelea kutoa huduma kwa wafugaji
ikiwemo kutoa chanjo kwa mifugo, usimamizi na ukaguzi wa nyama ili kuhakikisha
wananchi wanapata nyama safi na salama kwa ajili ya kulinda afya zao. Aliongeza
kuwa wafugaji wanaendelea kupewa elimu ya kuboresha koosaafu za mifugo yao na usajili ili waweze kuongeza tija ya uzalishaji
wa maziwa na kupunguza idadi ya mifugo na kukuwa kiuchumi. “Jumla ya ng’ombe 553 wamepandikizwa kwa chupa na ndama
walioboreshwa 405 wamepatikana.
Mheshimiwa Rais, wilaya imeweza kutoa elimu ya ufugaji wa samaki kwa wananchi
ambapo hadi sasa kuna mabwawa 137 ya
kufugia samaki yanayomilikiwa na wafugaji
95 na soko kubwa la samaki hao
ni ndani ya wilaya. Pia leseni 243 zimetolewa
kwa wafanyabiashara wa samaki ” alisema Mbugi.
Mwenge wa Uhuru Mwaka 2026 unaongozwa na kaulimbiu
isemayo ‘Tanzania ni Yetu Sote,
Tushikamane kwa pamoja Kuleta Maendeleo’.
MWISHO
Comments
Post a Comment