Shilingi 8,318,810,005 zatolewa kuboresha sekta ya Elimu Dodoma

Na. Dennis Gondwe, DODOMA

WILAYA ya Dodoma imepokea shilingi 8,318,810,005 kwa ajili ya kuboresha sekta ya elimu zikihusisha elimu bila malipo na ujenzi wa miundombinu ya elimu kwa ajili ya kuboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia.


Kauli hiyo ilitolewa na Katibu Tawala Wilaya ya Dodoma, Sakina Mbugi alipokuwa akisoma Risala ya Utii kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan wakati wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Wilaya ya Dodoma katika uwanja wa Shule ya Msingi Kizota jijini Dodoma.

Alisema kuwa katika kipindi cha Julai, 2025 hadi Aprili, 2026 Wilaya ya Dodoma ilipokea shilingi 8,318,810,005 kwa ajili ya kuboresha sekta ya elimu. Alisema kuwa kati ya fedha hizo, shilingi 3,777,397,654 ni kwa ajili ya elimu bila malipo kwa shule za Awali, Msingi na Sekondari na shilingi  4,541,412,351 kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu. ”Mheshimiwa Rais, kwa Kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia, ufaulu umepanda katika shule za msingi kutoka asilimia 93.2 mwaka 2024 hadi asilimia 94.3 mwaka 2025. Pia, jumla ya wanafunzi 13,971 wameandikishwa mwaka 2026 kujiunga na darasa la awali sawa na asilimia 71.9 na wanafunzi 21,724 darasa la kwanza sawa na asilimia 118.4. Aidha, katika shule za sekondari udahili wa wanafunzi wa Kidato cha Kwanza umeongezeka kutoka asilimia 89.6 mwaka 2025 hadi kufikia asilimia 93 mwaka 2026 na ufaulu umeongezeka kutoka asilimia 85.6 mwaka 2024 hadi asilimia 92.6 mwaka 2025” alisema Mbugi.

Alisema kuwa mwaka 2028 kutakuwa na wanafunzi wa kidato cha Kwanza waliomaliza darasa la Sita na darasa la Saba kwa pamoja. ”Hivyo, wilaya inatarajia kuwa na wanafunzi wa Kidato cha Kwanza 37,155. Kutokana na ongezeko hili, kwa Mwaka 2026/2027 wilaya imetenga shilingi 3,956,990,000 kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya madarasa, matundu ya vyoo pamoja na utengenezaji wa viti na meza kwa shule za sekondari” alisema Mbugi.

Mwenge wa Uhuru Mwaka 2026 unaongozwa na kaulimbiu isemayo ‘Tanzania ni Yetu Sote, Tushikamane kwa pamoja Kuleta Maendeleo ’.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wilaya ya Dodoma yapata “clean sheet” Miradi ya Mwenge wa Uhuru 2026