Ukarabati tanki la Maji Kata ya Ipala waleta neema kwa wananchi
Na. John Masanja, IPALA
Ukarabati
mradi wa tanki la maji la Lita 90,000 katika Kata ya Ipala, waleta ahueni kwa
wananchi na kuwapunguzia adha ya kutembea umbali mrefu kufuata maji kwa matumizi
mbalimbali.
Akizungumza na waandishi wa habari waliofanya ‘media tour’ kutembelea miradi ya maendeleo iliyotekelezwa na serikali katika Kata ya Ipala kuanzia mwaka 2021 hadi 2025, Diwani George Magawa aliishukuru serikali kwa kutoa fedha shilingi 43,406,300 kwaajili ya ukarabati wa tanki la mradi mkubwa wa Maji Ipala. “Wananchi sasa wanapata maji safi na salama. Kwahiyo, tunaishukuru serikali, tunamshukuru sana mbunge wetu na wataalam mbalimbali. Kata imechimba visima vinne kwaajili ya kupata maji safi na kupunguzia wananchi adha ya kutumia maji yasiyo salama. Hivi visima vinapunguza adha ya kwenda umbali mrefu kufuata maji ambayo mara nyingi siyo salama. Hivyo, wananchi wa kata yetu tatizo hili la uhaba wa maji limepungua sana” alisema Magawa.
Kwa upande
wake Mwenyekiti wa Bodi ya Maji Hombolo, Robison Mtolo, aliipongeza serikali
kwa kukarabati tanki hilo ambalo linahudumia wakazi zaidi ya 8,000 wa mitaa
mitano. Mtaa wa Azimio ukiwa na mradi wa pekee kutokana na jiografia ya eneo
hilo. “Mradi huu ni muhimu sana kwasababu umeondoa adha ya maji katika kata
yetu na watu wanayatumia hata kwa shughuli nyingine ndogo ndogo. Nawashukuru
wote tuliotumia umoja wetu kufanikisha mradi huu kukamilika na sasa watu
wanapata maji safi” alishukuru Mtolo.
Nae, mkazi wa Kata ya Ipala, David Mhuna alielezea furaha yake baada ya mradi huo wa maji kuboreshwa katani hapo. “Mimi nafurahishwa na mradi huu wa maji kwenye kata yetu ya Ipala, awali watu walikuwa wanateseka na kukesha kutafuta maji wakati mwingine wanakesha na hawapati maji. Kwasasa, maji ni mengi, tumevuta mabomba hadi majumbani mwetu. Tunasema asante sana kwa serikali na uongozi wote wa kata” alisema Mhuna.
MWISHO
Comments
Post a Comment