Sekondari Zuzu yapongezwa usimamizi na utunzaji Mazingira
Na. Mwandishi wetu, ZUZU
SHULE ya Sekondari Zuzu imepongezwa kwa
usimamizi mzuri wa shule na utunzaji wa mazingira jambo linalochochea utulivu
wakati wa kufundisha na kujisomea kwa wanafunzi.
Kauli hiyo ilitolewa na Mkuu wa Mkoa wa
Dodoma, Rosemary Senyamule alipotembelea na kukagua ujenzi wa mabweni mawili
katika Shule ya Sekondari Zuzu.
Mkuu wa mkoa alimpongeza Mkuu wa Shule
ya Sekondari Zuzu, kwa usimamizi mzuri wa shule hiyo. Alisema kuwa shule ina
mazingira safi na rafiki kwa wanafunzi kujifunzia kwa utulivu na walimu kuweza
kufundisha vizuri jambo lililopelekea shule hiyo kushika nafasi ya tisa kimkoa
miongoni mwa shule za serikali.
Kwa upande
wake Mkuu wa Shule ya Sekondari Zuzu, Mwl. Hezron Lupondo aliishukuru Halmashauri
ya Jiji la Dodoma kwa kuendelea kuwekeza katika sekta ya elimu kupitia
uboreshaji wa miundombinu ya shule.
“Ujenzi wa
mabweni haya mawili umetupa hamasa kubwa sisi walimu na wanafunzi. Mazingira
bora ya kujifunzia yanachangia kuongeza ari ya kufundisha na kujifunza. Hivyo,
tunaamini yatachochea kufanya vizuri zaidi kitaaluma,” alisema Mwl. Lupondo.
Mbunge wa Jimbo la Dodoma Mjini, Pachal
Chinyele alisema kuwa ameridhishwa na ubora wa mabweni yaliyojengwa katika
shule ya sekondari Zuzu akiyataja kuwa yamejengwa kwa viwango vinavyokidhi
mahitaji ya wanafunzi.
“Mabweni
haya ni ya kisasa na yatasaidia kutatua changamoto zilizokuwa zinawakabili
wanafunzi, hususan za malazi na usafiri. Haya ni mazingira yanayowapa nafasi
nzuri zaidi ya kujifunza na kufanya vizuri kitaaluma,” alisema Chinyele.
Mradi wa ujenzi wa mabweni mawili
katika Shule ya Sekondari Zuzu ulianza kutekelezwa tarehe 7 Aprili, 2025 ukiwa
umefikia asilimia 99 ya utekelezaji wake umegharimu jumla ya shilingi milioni
331.
Comments
Post a Comment