RC Senyamule apongeza ujenzi S/M Goba

Na. Mwandishi wetu, MKONZE

SHULE ya Msingi Goba iliyogharimu shilingi milioni 302 imeongeza fursa ya upatikanaji wa elimu bora kwa watoto na kuwapunguzia kutembea umbali mrefu kufuata shule katika maeneo mengine.



Kauli hiyo ilitolewa na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule alipotembelea na kukagua mradi wa ujenzi wa Shule ya Msingi Goba iliyopo Mtaa wa Muungano A, Kata ya Mkonze jijini Dodoma.

Mkuu wa mkoa aliipongeza Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwa kukamilisha mradi huo unaolenga kuongeza fursa za upatikanaji wa elimu bora kwa watoto.

Vilevile, aliipongeza Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwa utekelezaji mzuri wa mradi huo na kusisitiza umuhimu wa kuendelea kuwekeza katika miundombinu ya elimu ili kukidhi mahitaji yanayotokana na ongezeko la idadi ya watu.

Nawapongeza kwa kukamilisha ujenzi wa shule hii kwa wakati na kwa viwango vinavyohitajika. Hata hivyo, kutokana na kasi ya ukuaji wa Jiji la Dodoma, ni muhimu kuendelea kujenga miundombinu zaidi ya elimu ili kuhakikisha kila mtoto anapata mazingira bora ya kujifunzia," alisema Senyamule.

Alisema uwekezaji katika sekta ya elimu ni msingi wa kuandaa kizazi chenye maarifa na ujuzi. Juhudi za serikali za kuongeza shule na kuboresha mazingira ya kujifunzia zinapaswa kuendelea kupewa kipaumbele, aliongeza.

Akizungumza kwa niaba ya wakazi wa Mtaa wa Muungano A, Justine Mrema aliipongeza serikali kupitia Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwa ujenzi wa Shule ya Msingi Goba, akisema kuwa mradi huo umepunguza adha iliyokuwa ikiwakabili watoto kutembea umbali mrefu kufuata masomo katika Shule ya Msingi Mkonze.

“Kabla ya shule hii kujengwa, watoto wetu walilazimika kutembea umbali mrefu kila siku kwenda Shule ya Msingi Mkonze. Hali hiyo ilikuwa inawachosha na wakati mwingine kuchelewa kufika shuleni. Sasa tunaishukuru serikali kwa kutusogezea huduma hii muhimu, kwasababu watoto wetu watasoma katika mazingira salama na karibu na makazi yao,” alisema Mrema.

Mradi wa ujenzi wa Shule ya Msingi Goba ulianza tarehe 20 Novemba, 2025, umefikia asilimia 99 ya utekelezaji ukijenga vyumba nane vya madarasa, yakiwemo madarasa sita ya elimu ya msingi na mawili ya elimu ya awali, pamoja na jengo la utawala, matundu 10 ya vyoo kwa elimu ya msingi na matundu sita ya vyoo kwa elimu ya awali chini ya ufadhili wa Benki ya Dunia kupitia programu ya BOOST kwa gharama ya shilingi milioni 302.

 

Comments

Popular Posts

Jiji la Dodoma lashauriwa kulinda hadhi ya Makao Makuu ya Nchi

Afisa Biashara Arusha apongeza ukuwaji wa Biashara wa Jiji la Dodoma

Wakili Kipangula asisitiza weledi taaluma ya habari