Jiji la Dodoma kinara utekelezaji afua za Lishe
Na. Mwandishi wetu, DODOMA
HALMASHAURI ya Jiji la
Dodoma imepata alama ya kijani katika kadi alama ya viashiria vya utekelezaji
wa afua za lishe ikiwa ni hatua nzuri kwa kipindi cha Robo ya Nne kwa Mwaka wa
Fedha 2025/2026.
Akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa shughuli za Lishe kwa kipindi hicho, Kaimu Afisa Lishe wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Happiness Mlamka alisema kuwa utekelezaji umeendelea kufanyika kwa mafanikio makubwa ambapo kadi alama ya lishe imeonesha rangi ya kijani. Alisema kuwa rangi hiyo ni kiashiria kwamba halmashauri imefikia viwango vinavyotakiwa katika utekelezaji wa afua za lishe.
Akizungumza katika kikao
hicho, Mwenyekiti wake, Sakina Mbugi, aliyemuwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Dodoma
alipongeza Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwa kuendelea kufanya vizuri katika
utekelezaji wa shughuli za lishe. Alisisitiza umuhimu wa kuendeleza utoaji wa
elimu ya lishe kwa kutumia kaulimbiu mbalimbali zinazotolewa kupitia Mbio za
Mwenge wa Uhuru, ikiwemo “Zingatia lishe yako, imarisha afya, akili na utendaji
kazi”.
Aidha, aliwataka maafisa lishe
kuendelea kushirikisha makundi mbalimbali ya jamii, wakiwemo vijana, wazee,
viongozi wa dini na viongozi wa kimila, katika utoaji wa elimu kuhusu umuhimu
wa lishe bora ili kuongeza uelewa na kuimarisha afya za wananchi.
Mfumo wa tathimini, rangi ya kijani huonesha utekelezaji mzuri, rangi ya njano utekelezaji unaohitaji maboresho na ufuatiliaji zaidi na rangi nyekundu ikionesha kuna changamoto zinazohitaji hatua za haraka za kurekebisha.
Comments
Post a Comment