RC Senyamule aridhishwa maendeleo ya ujenzi Jengo Jumuishi Kituo cha Afya Makole
Na. Mwandishi wetu, DODOMA
HALMASHAURI ya Jiji la Dodoma
imepongezwa kwa usimamizi mzuri wa ujenzi wa mradi wa jengo jumuishi la Kituo
cha Afya Makole ukitajwa baada ya kukamilika kuwa utaboresha utoaji wa huduma
za afya kwa wananchi.
Pongezi hizo zilitolewa na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule alipofanya ziara ya kutembelea na kukagua maendeleo ya ujenzi wa jengo hilo jana.
Mkuu wa mkoa alisema kuwa kukamilika mradi
huo kutaleta mapinduzi makubwa katika utoaji wa huduma za afya katika
halmashauri. Alisema kuwa jengo hilo linajengwa eneo la kimkakati katikati ya
jiji likizungukwa na taasisi za serikali na binafsi.
“Jengo hili
litapanua huduma ambazo hazikuwepo hapo awali, ikiwemo huduma za dharura,
huduma za uzazi na huduma nyingine za kibingwa. Huu ni mradi muhimu ambao
utawawanufaisha wananchi wengi. Niwapongeze sana Halmashauri ya Jiji la Dodoma
kwa usimamizi mzuri,”
alisema Senyamule.
Alitumia wakati huo kuwapongeza watumishi
wa Kituo cha Afya Makole kwa kuendelea kutoa huduma bora zinazowavutia wananchi
licha ya uwepo wa hospitali nyingine nyingi jijini Dodoma.
“Idadi kubwa
ya wananchi, hususan wajawazito, wanaendelea kufika hapa kupata huduma kwa
sababu huduma zinazotolewa ni bora. Huduma bora ndiyo zinazojenga imani ya
wananchi na kuongeza idadi ya wanaofika kupata matibabu,” alisisitiza.
Comments
Post a Comment