Jiji la Dodoma latakiwa kushirikisha wadau afua za Lishe
Na. Mwandishi Wetu, DODOMA
HALMASHAURI ya Jiji la
Dodoma imetakiwa kuongeza ushirikishaji wa makundi mbalimbali ya jamii katika
kuimarisha afua za lishe ili kuhakikisha elimu na huduma za lishe bora
zinawafikia wananchi wote.
Wito huo ulitolewa na Mwenyekiti wa Kikao cha Tathmini ya Mkataba wa Lishe kwa Robo ya Nne Aprili-Juni, 2026 Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Sakina Mbugi alipoongoza kikao hicho kwa niaba ya mkuu wa wilaya kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa halmashauri.
Mbugi ambae ni katibu tawala wilaya ya Dodoma alisema kuwa ni
muhimu kuwashirikisha vijana waliopo nje ya mfumo rasmi, wazee, viongozi wa
dini, viongozi wa mila, taasisi za serikali na binafsi, watu mashuhuri pamoja na
kaya katika kuhamasisha na kutoa elimu ya lishe bora.
Alisema kuwa ushirikishwaji wa makundi
mbalimbali ya jamii ni muhimu katika kuongeza uelewa na kuleta matokeo chanya
na kubainisha kuwa lishe bora
haihusu
watoto pekee bali watu wa rika zote.
“Sisi, timu ya wataalam,
tupo tayari kuhakikisha kuwa makao makuu ya nchi yanazingatia lishe bora.
Jitihada za kuhimiza lishe bora zinaanza na mimi binafsi, kisha zinakufikia
wewe na hatimaye jamii kwa ujumla,” alisema Mbugi.
Naye, Kaimu Afisa Lishe wa Jiji la Dodoma, Happiness Mlamka alisema kuwa
utekelezaji
wa viashiria vya lishe kwa kipindi cha Mwezi Aprili hadi Juni, 2026 umeonesha
mafanikio makubwa. Alisema kuwa huduma muhimu za lishe zikiwemo utoaji wa
virutubisho na matibabu kwa watoto wenye utapiamlo zimefikia malengo
yaliyowekwa.
Comments
Post a Comment