Wananchi Kata ya Chang’ombe wahimizwa kulinda miundombinu
Na. Mwandishi Wetu, DODOMA
Wananchi wa Kata ya Chang’ombe watakiwa kuendelea
kuitunza na kuilinda miradi ya maendeleo ili iweze kutoa huduma kwa muda mrefu
na kuvinufaisha vizazi vya sasa na vijavyo.
Hayo aliyasema Naibu Meya wa Halmashauri ya Jiji la
Dodoma, Bakari Fundikira mara baada ya kutembelea na kukagua utekelezaji wa
miradi ya maendeleo katika Kata ya Chang’ombe jijini Dodoma.
Alisema kuwa serikali imeendelea kuwekeza fedha nyingi
katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo yenye lengo la kuboresha huduma za
kijamii na kuinua ustawi wa wananchi. “Hivyo, ni wajibu wa kila mwananchi
kushiriki katika kuilinda na kuitunza. Leo tumetembelea miradi mbalimbali
ikiwemo ujenzi wa Ofisi ya Mtaa wa Kishoka, Ofisi ya Mtaa wa Chang’ombe Juu,
Ofisi ya Mtaa wa Hamvu, kisima cha maji Shule ya Msingi Chang’ombe na
ujenzi wa Wodi ya Mama na Mtoto katika Kituo cha Afya
Chang’ombe ambapo miradi hii imejengwa kwa fedha za serikali jumla ya shilingi
456,926,355. Lakini pia nitoe rai kuwa ni muhimu kila mmoja wetu awe mlinzi wa
maendeleo haya kwa kuitunza, kuilinda na kuhakikisha inatumika kwa malengo
yaliyokusudiwa ili iendelee kuwanufaisha wananchi kwa miaka mingi ijayo,”
alisema Fundikira.
Aliongeza kuwa ushirikiano kati ya wananchi na serikali
ni msingi muhimu wa kuhakikisha uwekezaji unaofanywa unaendelea kuleta matokeo
chanya katika sekta mtambuka.
Kwa upande wake Afisa Mtendaji wa Kata ya Chang’ombe,
Hussein Kabezi alisema kuwa anaishukuru serikali kwa ujenzi wa miradi hiyo
kwasababu imekuwa na mchango mkubwa kwa maendeleo ya wananchi.
“Miradi hii imekuwa na mchango mkubwa katika kuboresha
upatikanaji wa huduma kwa wananchi na tunaahidi kuwa tutaendelea kushirikiana
na wakazi wa kata hii na kuhakikisha miundombinu yote inalindwa dhidi ya
uharibifu,” alisema Kabezi.
Comments
Post a Comment