Na. Dennis Gondwe, TAMBUKARELI

HALMASHAURI ya Jiji la Dodoma imetumia shilingi 519,891,609 kwa ajili ya kusimika mfumo wa kamera za usalama ili kuwahakikishia ulinzi na usalama wananchi na mali zao pamoja na wawekezaji.



Kauli hiyo ilitolewa na Mkuu wa Kitengo cha Teknolojia ya Habari na Mawasiliano Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Joseph Fungo alipokuwa akiwasilisha taarifa ya mradi wa kusimika kamera za usalama jijini Dodoma kwa Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa Mwaka 2026 tukio lililofanyika katika Hoteli ya Starline jijini Dodoma.

Akiongelea lengo la mradi huo, alisema kuwa ni kuimarisha ulinzi na usalama wa wananchi na mali zao. “Kamera hizi zinalenga kulinda miundombinu ya Umma katika Jiji la Dodoma, kudhibiti makosa ya barabarani na matendo ya uhalifu. Aidha, mradi utasaidia kutoa uhakika wa usalama kwa wadau wa shughuli za maendeleo na kulifanya Jiji la Dodoma kuwa salama kwa shughuli za uwekezaji, kidiplomasia, utalii na kuhakikisha Jiji linaendeshwa kidijitali” alisema Fungo.

Akiongelea gharama za mradi, alisema kuwa jumla ni shilingi 682,561,548. “Kati ya fedha hizo shilingi 519,891,609.27 zimetolewa na Halmashauri ya Jiji la Dodoma kupitia mapato ya ndani na shilingi 162,669,939.34 zimetolewa na Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote nchini Tanzania (UCSAF) ambazo zitalipwa kwa Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL), taasisi inayotekeleza jukumu la kuunganisha mfumo mzima wa kamera kupitia mkongo wa taifa” alisema Fungo.

Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa Wazo Mwang’onda aliipongeza Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwa kusimika kamera za usalama. Alisema kuwa kutokana na usimikaji wa mfumo huo, usalama ni mkubwa na kuwahakikishia wawekezaji kuwa watakuwa salama.

Alisema kuwa rai ya Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa wananchi wa Dodoma ni kulinda na kutunza amani ya nchi. Alisema kuwa maendeleo hayawezi kufanyika sehemu ambayo haina usalama na amani. “Mwenge wa Uhuru umetembelea mradi wa kamera za usalama na umefurahishwa sana na mradi huu” alisema Mwang’onda.

Nae mkazi wa Kata ya Tambukareli, Neema Wande alisema kuwa kamera za usalama zimesimikwa wakati muafaka ambapo Jiji la Dodoma linajitofautisha na maeneo mengine katika eneo la matumizi ya teknolojia kwa usalama wa watu na mali zao.

Mradi unatekelezwa na Kampuni ya Wisjane Smart Sytems ukiwa umefikia asilimia 80 ya utekelezaji.

MWISHO 

Comments

Popular Posts

Baraza la Madiwani Jiji la Dodoma lawafukuza kazi watumishi watatu na mmoja kushushwa cheo