Vijana watakiwa kuepuka matumizi ya Dawa za kulevya Dodoma
Na. Mwandishi wetu, DODOMA
VIJANA wahimizwa kuepuka matumizi ya dawa za kulevya
ambayo yanatajwa kuwa na madhara makubwa ili kulinda afya zao na kuchangia
maendeleo ya taifa.
Akizungumza katika Kongamano la Vijana lililofanyika
katika ukumbi wa Chuo cha Mipango na Maendeleo Vijijini (IRDP), Afisa
Mwandamizi kutoka Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya, Anna
Tengia alisema kuwa dawa za kulevya ni kemikali zinazobadilisha mfumo wa fahamu
wa binadamu na kuathiri mtu anavyofikiri na kutenda.
Aliweka mkazo kuwa vijana wajilinde ili kujenga kizazi
imara na kinachofikiria mustakabali bora wa maisha yao. “Dawa za kulevya
huathiri afya ya akili na mwili wa mtumiaji. Kwa maana hiyo hupunguza uwezo wa
vijana kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo” alisema Tengia.
Kwa upande wake, Afisa Sheria wa mamlaka hiyo, Meshak
Lyabonga wakati akitoa elimu alisisitiza kuwa matumizi ya dawa za kulevya ni
kosa la kisheria na wahusika wanaweza kuchukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria.
Kongamano hilo limeonesha umuhimu wa vijana kukutana na
kufanya mijadala muhimu ambayo itawasaidia katika kufanya maamuzi sahihi ili
kuepuka matumizi ya dawa za kulevya na kulinda afya zao.
MWISHO
Comments
Post a Comment