Jamii yatakiwa kuwajengea watoto utamaduni wa kupenda kupanda Miti na kuhifadhi Mazingira

 

Na. Dennis Gondwe, DODOMA

WADAU wa uhifadhi wa Mazingira wametakiwa kuwajengea watoto utaratibu wa kupanda miti na kupenda kudumisha usafi wa Mazingira katika maeneo yanayowazunguka ili kuwa na mandhari nzuri ya kuvutia.


Kauli hiyo ilitolewa na Katibu Tawala Mkoa wa Dodoma, Dkt. Khatibu Kazungu alipomuwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Dodoma katika zoezi la usafi wa Mazingira ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani lililofanyika katika Soko la wazi la Machinga jijini Dodoma.

Akizungumza na mamia ya wananchi waliojitokeza kushiriki zoezi hilo la usafi, alisema kuwa wadau wa masuala ya usafi na jamii kwa ujumla wana wajibu wa kuwafundisha na kuwarithisha watoto kupenda usafi na kuchukia mazingira machafu. “Pamoja na usafi, pia tuwakumbushe watoto wetu kupanda miti katika maeneo yanayotuzunguka. Kurithisha tabia ya kupenda kupanda miti inatuhakikishia mandhari nzuri inayotuzunguka na kuepuka tishio la mabadiliko ya tabia nchi” alisema Dkt. Kazungu.

Kwa upande wake, mwakilishi wa Mkurugenzi Msaidizi wa Mazingira kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais- Muungano na Mazingira, Martha Ngalowera alisema kuwa zoezi la usafi wa mazingira katika Soko la wazi la Machinga ni kuweka alama ya maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani.

Alisema kuwa maadhimisho hayo yanaongozwa na kaulimbiu isemayo ‘Dira 2050, tuwajibike kukijanisha Tanzania’. “Kupitia kaulimbiu hii tunatarajia ifikapo Mwaka 2050, Tanzania iwe kati ya nchi 10 bora katika uhifadhi wa mazingira. Kwa maana hiyo, kaulimbiu hii inalenga kuhamasisha jamii kuelekea Dira 2050” alisema Ngalowera.



Ikumbukwe kuwa maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani nchini yalianza tarehe 11 Mei na yanatarajiwa kuhitimishwa tarehe 5 Juni, 2026, baada ya Waziri mwenye dhamana na Mazingira kutoa tamko rasmi la serikali la maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani, yatakayokuwa pamoja na mambo mengine kuzindua programu kabambe ya kukijanisha Tanzania ikilenga kuifanya kuwa kinara wa uhifadhi wa Mazingira.

Comments

Popular Posts

Baraza la Madiwani Jiji la Dodoma lawafukuza kazi watumishi watatu na mmoja kushushwa cheo

Odero: Mwenge wa Uhuru alama ya Umoja Wilayani Dodoma