Vijana Dodoma watakiwa kutekeleza wajibu wao katika jamii

Na. Mwandishi Wetu, DODOMA

VIJANA wametakiwa kujitambua, kuthamini nafasi yao katika maendeleo ya taifa na kutekeleza wajibu kwa familia na jamii kwa ujumla ili kuchangia ustawi wa nchi.




Wito huo ulitolewa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Patrobas Katambi wakati akizungumza katika Kongamano la Vijana lililofanyika katika ukumbi wa Chuo cha Mipango na Maendeleo Vijijini (IRDP) katika Wilaya ya Dodoma ikiwa ni kuelekea mapokezi ya Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa Mwaka 2026 katika ya Wilaya ya Dodoma.

Alisema kuwa vijana wana nafasi kubwa katika kuendeleza amani, uzalendo na maendeleo ya taifa, hivyo wanapaswa kutumia fursa walizonazo kwa manufaa yao na ya jamii inayowazunguka. “Kuelekea Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa Mwaka 2026, ninawahimiza vijana wote kujitambua, kujua wajibu wao kwa familia, jamii na taifa kwa ujumla. Vijana ndiyo nguvu kazi ya taifa na msingi wa maendeleo endelevu” alisema Katambi.

Aliongeza kuwa Mwenge wa Uhuru unaendelea kuwa chombo muhimu cha kuhamasisha maendeleo, kudumisha umoja wa kitaifa na kuibua miradi yenye manufaa kwa wananchi, hivyo ushiriki wa vijana katika shughuli zake ni jambo la msingi.




Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Alhaj Jabir Shekimweri alitoa shukrani kwa waziri kuweza kushiriki katika kongamano hilo. “Kwanza kabisa nitoe pongezi zangu za dhati kwa waziri ambapo ameweza kuungana na sisi katika kongamano hili na kutoa nasaha zake na kuzungumza na vijana wa Wilaya ya Dodoma. Hivyo, nina imani kupitia mafunzo haya vijana hawa wataenda kuwa bora” alisema Alhaj Shekimweri.

Kongamano hilo lililenga kujadili nafasi ya vijana katika maendeleo ya taifa, kujenga uzalendo na kuhamasisha ushiriki wao katika shughuli mbalimbali za kijamii na kiuchumi kuelekea Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa Mwaka 2026 itakayofanyika tarehe 1 Juni, 2026.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Baraza la Madiwani Jiji la Dodoma lawafukuza kazi watumishi watatu na mmoja kushushwa cheo

Odero: Mwenge wa Uhuru alama ya Umoja Wilayani Dodoma