Waziri Mkuu amtaka Mkandarasi kukamilisha Soko Kuu la Majengo kwa wakati
Na. Nancy Kivuyo, DODOMA
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Nchemba atembelea Soko Kuu la Majengo
jijini Dodoma leo kwa ajili ya kukagua maendeleo ya ukarabati wa soko hilo na
kutoa maagizo kwa mkandarasi
anayekarabati soko hilo kuhakikisha
kazi inakamilika kwa wakati na kwa ubora unaostahili.
Katika ziara hiyo, Waziri Mkuu aliambatana na viongozi wa Mkoa wa Dodoma pamoja na Halmashauri ya Jiji la Dodoma ambapo alisomewa taarifa ya ukarabati wa miundombinu mbalimbali inayoboreshwa kama vile maeneo ya biashara, mitaro ya maji ya mvua, mifumo ya usalama na umeme.
Baada ya taarifa
hiyo, Waziri
Mkuu alisema kuwa serikali imejipanga kuhakikisha soko linarejea katika
matumizi haraka ili kuwezesha wananchi na wafanyabiashara kunufaika na
miundombinu bora. “Mradi huu ni muhimu sana kwa wananchi wa Dodoma na lazima
ukamilike kwa wakati na kwa kiwango bora. Mkandarasi hakikisha soko hili
linakamilika kama ambavyo mkataba unasema. Nanyi jiji naelekeza kuwa soko
litakapokamilika hawa wafanyabiashara waliokuwa hapo ndio wapewe kipaumbele na
sio vinginevyo. Tunatarajia kuwa mtasimamia vizuri pasiwepo malalamiko” alisema
Dkt. Nchemba.
Nae, Mbunge wa Jimbo la
Dodoma Mjini, Paschal Chinyele ambaye alihudhuria ziara hiyo, alimkaribisha
Waziri Mkuu na kueleza kuwa wafanyabiashara wanasubiri kwa hamu kukamilika kwa
soko hilo ili warejee kuendelea na shughuli zao. “Wafanyabiashara wetu
wanategemea soko hili kwa kipato chao cha kila siku. Wamevumilia kipindi cha
ukarabati na wanaomba likamilike kwa wakati. Pia baadhi ya barabara zimefungwa
kupisha ukarabati, hivyo wananchi wana matarajio makubwa” alisema
Chinyele.
Aidha, mbunge huyo aliiomba serikali kuangalia uwezekano wa kujenga maegesho ya magari katika eneo la korongo lililopo pembezoni mwa soko ili kuboresha zaidi mandhari na uendeshaji wa shughuli za kila siku. “Eneo lile lina nafasi nzuri kwa maegesho ya kisasa ambayo yatapunguza msongamano na kuongeza mpangilio mzuri wa biashara na soko letu kwa ujumla” aliomba Chinyele.
Katika hatua nyingine
mfanyabiashara wa Soko la Majengo, Rose Mtundu aliipongeza serikali kwa
jitihada za kuboresha soko hilo. “Tunashukuru kuona serikali inafuatilia
ukarabati huu kwa karibu. Soko likikamilika litakuwa msaada mkubwa kwa wananchi
na sisi wafanyabiashara. Tunatarajia patakuwa sehemu salama na penye mpangilio” alisema Mtundu.
Ziara
hiyo imeonesha matumaini
makubwa ya wananchi na viongozi kwamba Soko Kuu la Majengo litakuwa miongoni
mwa masoko ya kisasa na yenye kutoa fursa pana za kiuchumi kwa wakazi wa
Dodoma.
MWISHO
Comments
Post a Comment