Diwani Alimwoni Chaula, achaguliwa Meya Jiji la Dodoma

Na. Dennis Gondwe, DODOMA

Baraza la Madiwani la Halmashauri ya Jiji la Dodoma katika mkutano wake wa kwanza limemchangua Alimwoni Simon Chaula, Diwani wa Kata ya Makutupora kuwa Mstahiki Meya wa Jiji hilo kwa kupata kura za ndiyo 57 sawa na asilimia 100 ya kura zote zilizopigwa.



Akitangaza matokeo ya kura zilizopigwa, Mwenyekiti wa Mkutano wa Halmashauri, Sakina Mbugi alitangaza kuwa Diwani Alimwoni Chaula alipata kura 57 kati ya kura 57 zilizopigwa na wajumbe. “Niwapongeze wajumbe wote halali mlioshiriki kupiga kura kwa nafasi ya Mstahiki Meya na Naibu Meya. Naomba kutanga za matokeo kama ifuatavyo. Nafasi ya Mstahiki Meya, kura 57 zilipigwa, hakuna kura ambayo haikupigwa. Kura zote 57 ni kura za ndiyo. Kwa matokeo hayo, ninamtangaza rasmi Mheshimiwa Alimwoni Chaula kuwa Mstahiki Meya wa Jiji la Dodoma. Nafasi ya Naibu Meya, jumla kura zilizopigwa 55 kati ya kura 57. Wajumbe wawili hawakupiga kura. Kura za ndiyo ni zote 55. Hivyo, ninatangaza rasmi kuwa Mheshimiwa Bakari Fundikira ameshinda uchaguzi na amekuwa Naibu Meya wa Jiji la Dodoma. Hongera sana” alisema Mbugi.

Awali akiomba kura katika mkutano huo, Alimwoni Chaula alisema kuwa aliomba nafasi hiyo kwa sababu anao uwezo na ari ya kuitumikia halmashauri. “Nitashirikiana sana na wafanyakazi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, nitashirikiana sana na madiwani wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma kufanikisha ile dhima ya rais wetu, ya kazi na utu mbele. Nawaomba madiwani wenzangu kura za ndiyo, naomba tumalize kwa haki” alisema Chaula.

Katibu wa Mkutano wa kwanza wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Dkt. Frederick Sagamiko alisema kuwa baada ya uchaguzi mkuu, kata zote na madiwani wa viti maalum ushindi ulienda kwa Chama Cha Mapinduzi. Hivyo basi, katika uchaguzi huu tutakuwa na wawakilishi wa chama kimoja ambacho ni CCM. Tarehe 2 Desemba, 2025 nilipokea barua kutoka kwa Katibu wa CCM Wilaya ya Dodoma kuwasilisha jina la Mstahiki Meya na jina la Naibu Meya wa Jiji la Dodoma ili kuendelea na taratibu za kiserikali. “Alimwoni Simon Chaula amependekezwa kupombea nafasi ya Mstahiki Meya na Bakari Samwel Fundikira amependekezwa kugombea nafasi ya Naibu Meya wa Jiji la Dodoma” alisema Dkt. Sagamiko.

MWISHO

 

Comments

Popular Posts

Watumishi wa Kanda Namba Tatu watembelea Zahanati ya Soweto

Gari la Darasa Tembezi latoa elimu Mitaa ya Jiji la Dodoma