Madiwani watakiwa kuifanya Dodoma kuwa kinara ukusanyaji mapato

Na. Dennis Gondwe, DODOMA

MKUU wa Wilaya ya Dodoma, Alhaj Jabir Shekimweri amelitaka Baraza la Madiwani kuendelea kuifanya Halmashauri ya Jiji la Dodoma kuwa kinara katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo kupitia mapato ya ndani ili kuwaletea wananchi maendeleo na kuboresha maisha yao.



Kauli hiyo aliitoa alipokuwa akiwasalimia madiwani katika mkutano wa kwanza wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma uliofanyika katika ukumbi wa halmashauri jijini hapa.

Alhaj Shekimweri alisema “katika mapato ya ndani mmekuwa vinara katika kutekeleza miradi mizuri  ya maendeleo. Tumeona miradi ya hoteli, mradi wa Soko la wazi la Machinga, miradi ya ujenzi wa barabara, mfano ile ya Nala kuelekea hospitali ya jiji na miradi mingine mingi. Nendeni mkawe vinara wa kutekeleza miradi ya maendeleo. Ninayasema haya kwa kumuenzi Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwamba mnapochukua madaraka yale mema yaliyoanzishwa na wenzenu msiyaweke kando, ambayo hayajakamilika mkayakamilishe, yanayoendelea mkayakalishe huku mkianzisha mengine mapya”.

Nae, Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma alisema kuwa jiji lilikusanya jumla ya shilingi bilioni 22, 193,124,132.17  kwa kipindi cha Julai – Oktoba ambayo ni sawa na asilimia 30.9 ya lengo la mwaka.

Katika hatua nyingine, Diwani wa Kata ya Dodoma Makulu, Samson Mkopi alipongeza makusanyo yaliyopatikana na kuahidi kushirikiana na watendaji katika kanda ili kuongeza mapato. “Ndugu Mwenyekiti, tunapongeza sana makusanyo hayo, ni imani yetu kuwa tutatoa ushirikiano zaidi ili kuongeza ukusanyaji mkubwa wa mapato katika jiji letu ili mapato ya ndani yaweze kwenda kwa wananchi kutekeleza miradi ya maendeleo” alipongeza.

MWISHO

 

Comments

Popular Posts

Watumishi wa Kanda Namba Tatu watembelea Zahanati ya Soweto

Gari la Darasa Tembezi latoa elimu Mitaa ya Jiji la Dodoma