Madiwani Jiji la Dodoma watakiwa kuwa walezi

Na. Dennis Gondwe, DODOMA

MADIWANI wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma wametakiwa kutumia nafasi yao na kuwa walezi kwa maafisa watendaji katika kata zao na kuwasimamia ili kuwaletea maendeleo wananchi.


Rai hiyo ilitolewa na Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Alhaj Jabir Shekimweri alipokuwa akiongea na madiwani katika mkutano wa kwanza wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma baada ya Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani wa tarehe 29 Oktoba, 2025.

“Waheshimiwa Madiwani, nataka niwaombe sana mkawalee maafisa watendaji wenu kwenye ngazi ya kata. Mstahiki Meya, ninasema hapa kwa kuwaangukia na kuwaomba, mkawe walezi, ninyi ndiyo wenyeviti wa kamati za maendeleo kwenye kata, mkono wako wa kulia ni katibu, ambae ni Afisa Mtendaji wa Kata. Watendaji hawa inawezekana wakawa na madhaifu ya hapa na pale, nenda ukawe mlezi, nenda ukawe mzazi, yeye pamoja na wataalam wengine ngazi ya kata. Wasaidieni wafanye majukumu yao sawasawa ili wewe upate matokeo na kuwaletea wananchi maendeleo. Mimi, nitakusifu sana ukimkuta mtendaji ambae anachangamoto, ukamsaidia akaimarika kwenye changamoto yake, akawa mtendaji mzuri. Hivyo, kila mmoja akija hapa na kulalamika huyu mtendaji siyo mzuri, tumtoe, siyo mzuri mtoe, namtoa nampeleka wapi?, Nataka niwaombe sana, hata sisi wenyewe hatujakamilika…twende tukawajenge wafanye kazi zao vizuri ili watusaidie katika majukumu yetu kwenye kata zetu” alisema Alhaj Shekimweri.

MWISHO

 

Comments

Popular Posts

Watumishi wa Kanda Namba Tatu watembelea Zahanati ya Soweto

Gari la Darasa Tembezi latoa elimu Mitaa ya Jiji la Dodoma