M/Kiti CCM apewa kongole kuchagua safu makini ya madiwani

Na. Dennis Gondwe, DODOMA

MWENYEKITI wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Dodoma amepongezwa kwa kupanga safu makini ya wagombea nafasi ya udiwani jambo lililowawezesha kushinda kwa kishindo katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, 2025.



Pongezi hizo zilitolewa na Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Alhaj Jabir Shekimweri alipotoa salamu katika mkutano wa kwanza wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma uliofanyika katika ukumbi wa halmashauri.

Alhaj Shekimweri alisema “nichukue nafasi hii kuwapongeza waheshimiwa madiwani kwa kuchaguliwa kwa kishindo kuwa madiwani kwa kata zenu, ninyi mnatokana na CCM. Mstahiki Meya, nichukue nafasi hii kumpongeza Mwenyekiti, Charles Mamba kwa kuteua madiwani wazuri waliofanya kampeni zao kistaarabu na kuchaguliwa kwa kishindo kuunda Baraza la Madiwani la Jiji la Dodoma”.

Aidha, aliwapongeza wabunge wa Jimbo la Dodoma Mjini na Mtumba kwa kuchaguliwa kuwa wabunge. “Mstahiki Meya, ulikuwa ni Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani, nichukue nafasi hii kuwapongeza wabunge wetu, Mheshimiwa Chinyele na Mheshimiwa Mavunde pamoja na wale wa viti maalum wote. Wameshimiwa wabunge hongereni kwa kinyang’anyiro na hongereni kwa kuwa Madiwani wa Baraza la Madiwani la Jiji la Dodoma. Lakini pia, ulikuwa uchaguzi wa rais tunampongeza kwa dhati Dkt. Samia Suluhu Hassan ambae alipata ushindi wa kishindo wa karibu asilimia 97.7 na kuchaguliwa kuwa rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania” alisema Alhaj Shekimweri.

Katika hatua nyingine, Mstahiki Meya Jiji la Dodoma, Alimwoni Chaula alishukuru kwa kuchaguliwa kuwa Mstahiki Meya wa Jiji la Dodoma na kuahidi kufanya kazi kwa kushirikiana na baraza la madiwani ili kuongeza kasi ya maendeleo kwa wananchi.

Alisema kuwa vipo vipaumbele muhimu atakavyoanza navyo katika kuhakikisha jiji linasonga mbele. “Vipo vipaumbele muhimu kama vile kusimamia masuala ya ardhi, kusimamia mapato, mikopo ile ya makundi maalum tunaelewa tuna vijana ambao wanahitaji kukuza uchumi wao binafsi. Kuna masuala ya elimu na maji, vyote hivyo tutaenda kuvisimamia kwa weledi mkubwa” alisema Chaula.

Nae, Diwani wa Kata ya Madukani, Prof. Davis Mwamfupe alisema kuwa anawapongeza madiwani wenzake kwa kufanikisha uundaji wa Baraza jipya la Madiwani. “Natoa pongezi kwetu sote, nina imani baraza hili litakwenda kuwa bora na la kipekee kwasababu unaona idadi kubwa ya waliochaguliwa ni vijana. Vijana wana nguvu, ari na mwamko wa kuchapa kazi” alisema Prof. Mwamfupe.

MWISHO

 

Comments

Popular Posts

Watumishi wa Kanda Namba Tatu watembelea Zahanati ya Soweto

Gari la Darasa Tembezi latoa elimu Mitaa ya Jiji la Dodoma