DC Shekimweri asisitiza semina elekezi kwa madiwani Dodoma

Na. Dennis Gondwe, DODOMA

MKUU wa Wilaya ya Dodoma, Alhaj Jabir Shekimweri amesema kuwa semina elekezi kwa madiwani wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma ni muhimu ili kuwapa maarifa na kufanya uendeshaji wa mikutano ya halmashauri kuwa ya viwango kwa mujibu wa kanuni zilizopo.



Kauli hiyo aliitoa alipokuwa akiwasalimia madiwani katika mkutano wa kwanza wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma baada ya Uchanguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani wa tarehe 29 Oktoba, 2025.

“Ninawapongeza kwa dhati Mstahiki Meya, Chaula na Naibu Meya, Fundikira kwa kuchaguliwa kwa kura nyingi na baraza hili. Ninyi bado ni vijana, kwa hiyo baraza hili lina sura ya viongozi wa vijana. Ukiangalia waheshimiwa madiwani wengi pia ni vijana, hapo peke yake ni fursa lakini pia ni changamoto msipoangalia vizuri. Nami niungane na mtoa hoja wa kwanza, kwamba yakaandaliwa mafunzo na kupata semina elekezi ili msheheni maarifa, uelewa wa taratibu za vikao, lakini kanuni za kudumu za Baraza la Madiwani. Kwa sababu katika mkutano huu mara zote ni kuzingatia sheria, kanuni, taratibu na miongozo ya nchi, siyo nje ya hapo. Dunia ya leo maarifa yanapatikana kwa njia nyingi na rafiki, njia nyepesi ya kwanza wapo madiwani wazoefu na wengine wana vipindi viwili hadi vitatu. Mpo na Mstahiki Meya Mstaafu Prof. Mwamfupe na wengine wanaweza kushea. Lakini maarifa mengine yapo kwenye mtandao tu, nina fahamu kuna utaratibu wa kuwapatia vishikwambi kwa ajili ya uratibu wa vikao na taarifa za vikao. Mnaweza kuwawekea nyaraka hizo wakaanza kuzisoma taratibu. Nasema haya kwa sababu mnabeba matajio makubwa ya wakazi wa Dodoma” alisema Alhaj Shekimweri.

Aliwataarifu kuwa matarajio ya wananchi ni kuona kasi ya ufuatiliaji wa miradi ya maendeleo, utendaji wa jiji na utoaji wa huduma bora ikiongezeka. “Nawapongeza wote mliochaguliwa kuwa wenyeviti wa kamati za kudumu pamoja na wajumbe, kazi nyingi zitaanzia kwenye kamati zetu. Tunategemea kupata huduma bora kwenye sekta za afya, elimu, umeme, maji barabara, yote haya wananchi wanawaangalia ninyi. Nendeni mkatekeleze kwa kuzingatia Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya Mwaka, 2025-2030” alisema Alhaj Shekimweri.

MWISHO

 

Comments

Popular Posts

Watumishi wa Kanda Namba Tatu watembelea Zahanati ya Soweto

Gari la Darasa Tembezi latoa elimu Mitaa ya Jiji la Dodoma