Prof. Mohamed ahimiza wanafunzi kusoma kwa bidii na kuwapongeza wazazi

Na. Mwandishi Wetu, DODOMA

Wanafunzi wa Shule ya Sekondari Makutupora watakiwa kuwa na nidhamu na kusoma kwa bidii ili kufikia malengo yao ya kielimu na maisha kwa ujumla.



Hayo aliyasema Katibu Mtendaji Baraza la Mitihani la Tanzania, Prof. Said Mohamed wakati wa Uzinduzi wa Upandaji Miti mwaka 2025/2026 uliofanyika katika Shule ya Sekondari Makutupora Jijini Dodoma.

Alisema kuwa juhudi za wanafunzi katika masomo ni msingi muhimu wa maendeleo yao binafsi na taifa kwa ujumla. “Msingi mzuri wa watoto ni kupata elimu hivyo niwasihi wanafunzi muendelee kusoma kwa bidii ili kuweza kufikia ndoto zenu, kwasababu hapa kuna viongozi wa baadae ambao wataweza kuongoza taifa letu, lakini pia muwe na nidhamu kwasababu nidhamu ndio hupelekea kufika mbali hususan katika masomo yenu” alisema Prof. Mohamed.

Aidha aliwapongeza wazazi kwa juhudi wanazozifanya katika malezi ya watoto. “Nipende kuwapongeza wazazi kwa namna ambavyo mnaendelea kuwalea watoto katika misingi bora, lakini pia nisisitize ushirikiano kati ya wazazi pamoja na walimu kwasababu ushirikiano ni nguzo muhimu katika kufanikisha elimu bora kwa watoto” alisema Prof. Mohamed.



Kwa upande wake Mkuu wa Shule ya Sekondari Makutupora, Mwl. Didas Ndalu alimshukuru Katibu Mtendaji kwa kutembelea shule hiyo akieleza kuwa ujio wake ni faraja kubwa kwa wanafunzi na walimu. “Ni heshima kubwa kwetu kumpokea kiongozi huyu muhimu. Tunatarajia kuendelea kuinua kiwango cha taaluma na kuhakikisha wanafunzi wanapanda daraja mwaka hadi mwaka. Kutokana na walimu kuendelea kusimamia nidhamu ya wananfunzi ufaulu umeendelea kuongezea ikiwa kwa mwaka 2025 shule ilifaulu kwa GPA ya 3.4842, lakini pia tunaendela kuweka mikakati ya kuhakikisha tunafuta daraja sifuri na nne” alisema Mwl. Ndalu

Nae mzazi alieshiriki katika uzinduzi wa upandaji miti, Phatina Mbeyu alisema wazazi wataendelea kushirikiana na walimu katika kuhakikisha watoto wanalelewa katika maadili mema.  “Malezi bora kwa mtoto yanachangia kwa kiasi kikubwa mafanikio katika masomo yao. Hivyo, ni jukumu la kila mzazi kumsimamia mtoto katika malezi bora lakini pia ushirikiano wa karibu baina ya mzazi na Mwalimu humjenga mtoto na tutaendelea kushirikiana na walimu ili kuhakikisha wanafunzi wanazingatia elimu na kuwa na nidhamu” alisema Mbeyu.




Uzinduzi huo wa upandaji miti ni juhudi za kuhifadhi mazingira sambamba na kuhamasisha jamii umuhimu wa utunzaji mazingira na kupanda miti.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wanawake watakiwa kulipa kodi na kukuza uchumi katika Jiji la Dodoma

Jiji la Dodoma kuchangamkia fursa ujio wa Bandari Kavu Ihumwa

Watumishi wa Kanda Namba Tatu watembelea Zahanati ya Soweto