Waziri Mavunde akabidhi vifaa vya Michezo UMISETA Dodoma
Na. Mwandishi wetu, DODOMA
Wanafunzi wanaojiandaa kushiriki mashindano ya Umoja wa Michezo na Taaluma kwa
Shule za Sekondari Tanzania (UMISETA) ngazi ya mkoa wamepata hamasa mpya baada
ya kupokea vifaa vya michezo vilivyotolewa na Mbunge wa Jimbo la Mtumba na Waziri wa Madini,
Anthony Mavunde.
Vifaa hivyo vilikabidhiwa katika Shule ya Sekondari Dodoma kwa niaba ya Mbunge huyo kupitia Katibu wake, Silas Makanyaga, ambae alisema kuwa Jiji la Dodoma kupitia Ofisi ya Afisa Elimu Sekondari liliwasilisha ombi la vifaa vya michezo kwa ajili ya mashindano ya UMMISETA ngazi ya wilaya na mkoa, ambapo Mbunge amejitoa kusaidia kwa kununua jezi kwa kila mchezo.
“Tunawaomba vijana wetu kucheza kwa nidhamu, kuwasikiliza walimu wao na kuendelea kufanya vizuri kama ilivyo desturi ya Jiji la Dodoma ambalo limeendelea kuwa kinara kwa ushindi wa makombe mbalimbali” alisema Makanyaga.
Kwa upande, Afisa Elimu Sekondari Jiji la Dodoma, Mwl. Daniel Mapilya alisema kuwa tayari wanafunzi 120 kutoka shule mbalimbali za sekondari wamewasili kambini tangu Juni 5 kwa ajili ya maandalizi ya mashindano ya ngazi ya mkoa yaliyotarajiwa kuanza rasmi Juni 8 mwaka huu.
“Vijana hao wameonyesha utayari
mkubwa wa kushiriki na kuonesha ushindani wa hali ya juu. Tumepokea vifaa
mbalimbali ikiwemo jezi ambazo zimeongeza ari na furaha kwa wanafunzi wetu.
Tunamshukuru sana Mheshimiwa Mbunge kwa kuendelea kusimama nasi na mchango wake
mkubwa katika maendeleo ya michezo” alisema Mwl. Mapilya.
Sambamba na hilo, Afisa Michezo katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Peter
Ititi alisema kuwa vifaa vilivyotolewa vimeongeza morali na hamasa kwa
wanamichezo, akibainisha kuwa kwa miaka minne mfululizo mbunge huyo amekuwa
akiwaunga mkono kwa kutoa vifaa vya michezo jambo lililosaidia kuongeza
ushindani na mafanikio.
Nae, mchezaji wa mchezo wa kurusha tufe na Mpira wa Pete, Munira Mohamed
alisema kuwa vifaa walivyopokea kutoka kwa mbunge vimeongeza hamasa na kuwapa
nguvu ya kupambana kwa ushindi.
Hata hivyo, Nahodha wa timu ya mpira wa miguu, Gabriel Peter alisema kuwa timu
ipo katika maandalizi mazuri na watapeperusha vizuri bendera ya Jiji la Dodoma
kwa kurudi na ushindi mnono wa makombe kama zawadi ya shukurani kwa mbunge.
Mashindano ya UMISETA ngazi ya mkoa kwa Jiji la Dodoma yanashirikisha michezo
mbalimbali ikiwemo mpira wa miguu (football), mpira wa pete (Netball), mpira wa
kikapu (Basketball), mpira wa mikono (Handball), mpira wa wavu (Volleyball),
riadha, sanaa za ndani, muziki wa kizazi kipya, tenisi ya mezani (Table
Tennis), Goalball, kwaya na ngoma za asili.
Comments
Post a Comment